Thursday, August 15, 2013

KANU ANAAMINI NCHI YAKE NIGERIA INA UWEZO MKUBWA"

Mshambuliaji wa zamani Arsenal, Nwankwo Kanu, anaamini Nchi yake Nigeria inao uwezo wa kufuzu kucheza Fainali za Kombe la Dunia huko Brazil Mwaka 2014 na pia kufanya vyema.
Kanu amesema lengo lao ni kutwaa Ubingwa wa Dunia Mwaka 2014 kwa ajili ya Afrika.
Hadi leo hakuna Nchi hata moja ya Afrika iliyoweza kutinga Nusu Fainali za Kombe la Dunia na katika Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka 2010 huko Nchini Afrika Kusini, Ghana ilikosa kidogo kuwa Nchi ya kwanza kuingia Nusu Fainali ilipofanyiwa ukatili na Luis Suarez pamoja na Uruguay yake.
Kanu, aliewahi kuzichezea Klabu za Portsmouth, Arsenal, Inter Milan na Ajax, anaamini Nigeria, ambao ndio Mabingwa wa Afrika, wanayo Timu imara na Benchi la Makocha mahiri ambalo linaweza kuiwezesha Nchi hiyo kufuzu kwenda Brazil na kuonyesha maajabu.
Kanu, mwenye Miaka 37, alisema: “Ni wazi tutafika Fainali za Kombe la Dunia Mwakani na tunataka kutwaa Kombe kwa ajili ya Afrika. Bado tuna Mechi na Malawi na tuko tayari na tutafanya kila tuwezalo.”
Baada ya kutwaa Ubingwa wa Afrika Mwezi Januari, Nigeria waliiwakilisha Afrika kwenye Mashindano ya FIFA ya Kombe la Mabara huko Brazil Mwezi Juni lakini waliishia hatua ya Makundi tu waliposhindwa kufuzu toka Kundi lao lililokuwa na Timu za Spain, Uruguay na Tahiti.
Ili kufika Fainali za Kombe la Dunia huko Brazil Mwaka 2014, Nigeria wanahitaji kutofungwa Mechi ya Nyumbani ya mwisho ya Kundi lao dhidi ya Malawi hapo Septemba 7 na kisha kuifunga Timu watakayopangiwa kwenye Raundi ya Mwisho ya Mtoano ambapo zitachezwa Mechi mbili za Nyumbani na Ugenini.
Wakati huo huo, hapo Jana huko Moses Mabhida Stadium Nchini Afrika Kusini, Nigeria waliwafunga Afrika Kusini Bao 2-0 na kutwaa Taji la Nelson Mandela Challenge huku Bao zote zikifungwa Kipindi cha Pili na Uche Nwofor alietokea Benchi.

YANGA, AZAM KUVAANA NGAO YA JAMII J’MOSI

Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom, Yanga na makamu bingwa Azam wanavaana keshokutwa (Jumamosi) kwenye mechi ya Ngao ya Jamii (Community Shield) kuashiria uzinduzi wa msimu mpya wa 2013/2014.

Mechi hiyo inayotarajiwa kuwa kivutio kwa wapenzi wa mpira wa miguu nchini itachezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10.30 jioni ambapo mshindi atakabidhiwa ngao.


Iwapo dakika 90 za mechi hiyo hazitatoa mshindi, timu hizo zitatenganishwa kwa mikwaju ya penalti huku asilimia 10 ya mapato ya mechi hiyo yakienda kwa kituo cha kulelea watoto cha SOS.


Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 7,000 kwa viti vya rangi ya kijani na bluu wakati viti vya rangi ya chungwa ni sh. 10,000. Watakaiongia viti vya VIP C watalipa sh. 15,000, viti vya VIP B ni sh. 20,000 wakati VIP A watalipa sh. 30,000.

LIGI DARAJA LA KWANZA KUANZA SEPT 14

Michuano ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inayoshirikisha timu 24 zilizogawanywa katika makundi matatu msimu huu (2013/2014) itaanza kutimua vumbi Septemba 14 mwaka huu.


Kila timu itakayoongoza kundi lake katika ligi itakayochezwa kwa mikondo miwili (nyumbani na ugenini) ndiyo itakayopanda daraja kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu wa 2014/2015.


Mechi za ufunguzi kwa kundi A zitakuwa kati ya Tessema vs Green Warriors (Uwanja wa Karume, Dar es Salaam) wakati Septemba 15 mwaka huu ni Transit Camp vs Polisi Dar (Uwanja wa Mabatini, Pwani), Ndanda vs Friends Rangers (Uwanja wa Nangwanda, Mtwara) wakati Villa Squad vs African Lyon itachezwa Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.


Kundi B ni Burkina Faso vs Polisi Moro (Uwanja wa Jamhuri, Morogoro), Mkamba Rangers vs Lipuli (Uwanja wa CCM Mkamba, Morogoro), Majimaji vs Mlale JKT (Uwanja wa Majimaji, Songea) wakati Septemba 15 mwaka huu Kimondo SC vs Kurugenzi (Uwanja wa Sokoine, Mbeya).


Mechi za ufunguzi kundi C ni Polisi Mara vs Polisi Dodoma (Uwanja wa Karume, Musoma), Kanembwa JKT vs Polisi Tabora (Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma), Stand United vs Mwadui (Uwanja wa Kambarage, Shinyanga), na Pamba vs Toto Africans (Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza).


Mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo utamalizika Oktoba 26 mwaka huu wakati wa pili utamalizika Machi 22 mwakani. (Ratiba imeambatanishwa)


Boniface Wambura

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

RIBERY AWAHI KUFIKIRIA KUICHEZEA BARCELONA PAMOJA NA REAL MADRID"

Winga wa club ya Bayern Munich, Franck Ribery amekiri kuwahi kufikiria kuihama klabu hiyo na kwenda Barcelona katika kipindi cha majira ya kiangazi mwaka 2009 lakini aliamua kuheshimu mkataba wake na kubakia. Winga huyo wa kimataifa wa Ufaransa pia alikuwa akihusishwa na kutaka kusajiliwa na Real Madrid miaka michache iliyopita lakini sasa ameweka wazi kuwa Madrid sio klabu pekee iliyokuwa ikimhitaji nchini Hispania. 

Ribery amedai kuwa mchezaji mwenzake wa timu ya taifa ya Ufaransa, Eric Abidal ambaye alikuwa akicheza chini ya Pep Guardiola akiwa Barcelona alimfuata na kumwambia suala hilo katika msimu wa 2008-2009. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 30 alikiri kufikiria kujiunga na klabu hiyo kwa kipindi hicho kwasababu walikuwa na kikosi bora duniani. Ribery aliendelea kudai kuwa alikuwa katika kipindi kigumu kufanya uchaguzi lakini kwasababu ya umuhimu wa Karl-Heinz Rummenigge na Uli Hoeness ambaye ndiye rais wa klabu hiyo kwake aliamua kuheshimu mkataba wake na kutulia.