Friday, April 25, 2014

MAJARIBIO YA AZAM ACADEMI YASOGEZWA MBELE".

MAJARIBIO ya kusaka vipaji vya kujiunga na akademi ya Azam FC ambayo hufanyika kila tarehe ya mwanzo ya mwezi, hayatakuwepo kwa miezi ya Mei na Juni, mwaka huu.
Kocha Mkuu wa Azam Academy, Vivek Nagul raia wa India amesema majaribio yafuatayo yatafanyika Julai 1 mwaka huu kuanzia Saa 12.30 asubuhi Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
Vivek ameomba radhi kwa usumbufu wowote utakaojitokeza na amewataka vijana wenye ndoto za kujiunga na akademi hiyo kujitokeza Julai 1 kujaribu bahati yao. “Wazazi pia, ambao wana ndoto za kuwaleta vijana wao hapa, tunapenda kuwaambia nafasi nyingine kwao ni Julai 1, wanakaribishwa,”alisema.

MIAKA 20 WA KENYA WATUA KUIVAA NGORONGORO HEROES

TIMU ya vijana ya Kenya inatarajiwa kuwasili nchini leo (Aprili 25 mwaka huu) saa 1 usiku tayari kwa ajili ya mechi dhidi ya Tanz

ania (Ngorongoro Heroes).
Mechi hiyo ya marudiano ya michuano ya Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 itachezwa Jumapili (Aprili 27 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 2,000 na sh. 5,000.

Kenya na Ngorongoro Heroes zilitoka suluhu katika mechi ya kwanza iliyochezwa Machakos wiki tatu zilizopita.
Mshindi baada ya mechi ya marudiano atacheza na Nigeria katika raundi itakayofuata.
Ngorongoro Heroes inaendelea kujinoa kwa ajili ya mechi hiyo chini ya Kocha John Simkoko. Mechi hiyo itachezeshwa na waamuzi kutoka Burundi wakiongozwa na Pacifique Ndabihawenimana wakati Kamishna ni Tarig Atta Salih kutoka Sudan.

TAIFA STARS VS BURUNDI MAKOSHA WAAHINDI SOKA SAFI

MAKOCHA wa timu za Taifa za Tanzania (Taifa Stars) na Burundi (Intamba Mu Rugamba), Salum Mayanga na mwenzake Niyungeko Alain Olivier wameahidi burudani ya nguvu kwenye mechi yao itakayochezwa kesho (Aprili 26 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mechi hiyo ya kirafiki ambayo ni sehemu ya maadhimisho ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar itachezeshwa na refa Anthony Ogwayo kutoka Kenya na itaanza saa 10 kamili jioni.
Ogwayo atasaidiwa na Gilbert Cheruiyot na Oliver Odhiambo wote pia kutoka Kenya.

Mwamuzi wa mezani atakuwa Israel Mujuni wa Tanzania wakati Kamishna ni Charles Ndagala.
Mayanga amesema wanatumia mechi hiyo kama sehemu ya maandalizi ya mechi za mchujo za Kombe la mataifa ya Afrika, na ameahidi kuchezesha baadhi ya wachezaji waliopatikana kwenye mpango wa maboresho ya Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager.
Naye Niyungeko amesema amekuja na kikosi imara ambacho pia kitakuwa na washambuliaji wa Simba, Amisi Tambwe na Didier Kavumbagu wa Yanga, lengo lao ni kuhakikisha wanapata ushindi kwa vile Taifa Stars imekuwa ikiwasumbua kila wanapokutana nayo.

Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani. Kwa VIP A kiingilio kitakuwa sh. 20,000 wakati VIP B na C ni sh. 10,000.

Wakati huo huo, Kocha Mkuu mpya wa Taifa Stars, Martinus Ignatius Maria maarufu kama Mart Nooij atatambulishwa kwa waandishi wa habri kesho Jumamosi (Aprili 26 mwaka huu) saa 8 kamili mchana kwenye ukumbi wa mikutano wa Uwanja wa Taifa.