Friday, April 12, 2013

UJUMBE WA FIFA KUWASILI APRILI 15
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linapenda kuwatangazia wadau wa mpira wa miguu kuwa ujumbe wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) utawasili nchini Jumatatu (Aprili 15 mwaka huu) kwa ajili ya kushughulikia mchakato wa uchaguzi mkuu wa TFF.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka FIFA, ujumbe huo utaongozwa na Mkuu wa Idara ya Uanachama ya FIFA, Primo Covarro na utafanya kazi kwa siku tatu kuanzia siku ya ujio na kuondoka Aprili 18 mwaka huu.

Ukiwa nchini, ujumbe huo utakutana na wagombea uongozi walioathiriwa na uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF ambao waliomba mashauri yao yaangaliwe upya, wagombea ambao walikata rufani FIFA, Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Kamati ya Rufani na Sekretarieti ya TFF.

Wajumbe hao wangependa kukutana na waziri anayehusika na michezo, hivyo TFF imeiandikia Wizara ikipendekeza kuwa ujumbe huo ukutane na Waziri na wakuu wengine wa michezo Aprili 16 mwaka huu 2013 kabla ya kuanza kazi zao.

Wagombea watakaosikilizwa na ujumbe huo wa FIFA ni:
1.   Farid Salim Mbaraka Nahdi: Mgombea wa nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ambaye alienguliwa na Kamati ya Uchaguzi na baadaye rufani yake kwa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF kutupwa na hali kadhalika ombi lake la kutaka shauri lake liangaliwe upya, kukataliwa.

2.   Elliud Peter Mvella: Mgombea wa nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ambaye alikatwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF na kukata rufani Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF kabla ya maombi yake ya kutaka shauri lake kuangaliwa upya, kukataliwa.


3.   Mbasha Matutu: Mgombea wa nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ambaye alikatwa na Kamati ya Uchaguzi na kukata rufani ambayo pia ilitupwa kabla ya kuomba shauri lake liangaliwe upya, ombi ambalo lilikataliwa.

4.   Hamad Yahya: Mgombea wa nafasi ya uenyekiti wa Bodi ya Ligi ambaye alipitishwa na Kamati ya Uchaguzi, lakini mwekaji pingamizi akakata rufani ambayo ilikubaliwa na Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF na kuondolewa. Aliomba shauri lake liangaliwe upya, lakini Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF ikatupa ombi lake.

5.   Jamal Emily Malinzi: Mgombea wa nafasi ya urais wa TFF ambaye alipitishwa na Kamati ya Uchaguzi, lakini mwekaji pingamizi akakata rufani ambayo ilikubaliwa na Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF, hivyo kuondolewa kwenye mchakato. Aliomba shauri lake liangaliwe upya, lakini likakataliwa. Hata hivyo, alikuwa ameshakata rufani FIFA.

6.   Michael Wambura: Mgombea wa nafasi ya Makamu wa Rais wa TFF ambaye alikatwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF na rufani yake kukataliwa na Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF. Hakuomba shauri lake liangaliwe upya, lakini alikata rufani FIFA.

Shirikisho linawaomba wote waliotajwa hapo juu kujiandaa kwa utetezi na maelezo ya kutosha na kwamba barua za kuwaita zinafuata. (Orodha ya waathiriwa na programu ya ujumbe wa FIFA imeambatanishwa)

YANGA, OLJORO KUUMANA MECHI ZA VPL
Ligi Kuu ya Vodacom inaendelea kesho (Aprili 13 mwaka huu) kwa mechi mbili zitakazochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, na Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Yanga itakuwa mwenyeji wa Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Taifa wakati Uwanja wa Sokoine utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Tanzania Prisons na Ruvu Shooting.

Ligi hiyo itaendelea keshokutwa (Aprili 14 mwaka huu) kwa mechi kati ya wenyeji Azam na Simba. Mechi hiyo namba 155 itachezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

WASHELISHELI KUICHEZESHA AZAM CAF
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Shelisheli kuchezesha mechi ya kwanza ya raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho kati ya Azam na AS FAR ya Morocco itakayofanyika Aprili 20 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Waamuzi hao ni Emile Fred atakayepuliza filimbi akisaidiwa na Steve Maire na Jean Ernesta. Mwamuzi wa mezani (fourth official) atakuwa Jean Claude Labrossa. Kamishna wa mechi hiyo ni Abbas Sendyowa kutoka Uganda.

Wakati huo huo, CAF imemteua Mtanzania Alfred Lwiza kuwa Kamishna wa mechi ya kwanza ya raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho kati ya Liga Muculmana ya Msumbiji na Wydad Casablanca ya Morocco.

Mechi hiyo itakayochezwa kati ya Aprili 19,20 au 21 mwaka huu nchini Msumbiji itachezeshwa na waamuzi kutoka Zimbabwe wakiongozwa na Ruzive Ruzive.


Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Wednesday, April 10, 2013

KOCHA RHINO APIGWA FAINI, AFUNGIWA MECHI SITA
KAMATI ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imempiga faini ya sh. 400,000 na kumfungia mechi sita Kocha wa Rhino Rangers, Renatus Shija kwa kushiriki vitendo vinavyoashiria imani za ushirikina na kumdhihaki mwamuzi kwenye mechi za Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

Adhabu hizo zimetolewa kwa mujibu wa kifungu cha 31(1)(a) na (b) cha Kanuni za FDL ambapo Kocha huyo aliyeipandisha daraja Rhino Rangers kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) alifanya vitendo hivyo kwenye mechi mbili tofauti.

Mechi hizo ni kati ya Kanembwa JKT na Rhino Rangers iliyochezwa Februari 23 mwaka huu Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma, na ile kati ya Rhino Rangers na Morani iliyochezwa Machi 17 mwaka huu Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.

Pia klabu ya Rhino Rangers imepigwa faini ya sh. 200,000 kutokana na Polisi Wanajeshi- MP kuwapiga walinzi milangoni kwenye mechi hiyo dhidi ya Kanembwa JKT ili kupisha washabiki wa timu hiyo waingie bure uwanjani.

Mchezaji wa timu ya Pamba ya Mwanza, Leonard Nahole amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi nne baada ya kumrushia chupa ya maji mwamuzi kwa madai amependelea kwenye mechi dhidi ya Polisi Tabora iliyochezwa Machi 16 mwaka huu.

Nao wachezaji Joseph Mapalala, Yohana Mirobo, Noel Makunja, Mkome Pastory na Rudenzi Kilinga wa Polisi Mara wamepigwa faini ya sh. 200,000 kila mmoja na kufungiwa mechi tatu kwa kufanya vitendo vinavyoshiria ushirikina na kumkimbiza mwamuzi kwenye mechi dhidi ya Morani iliyochezwa Machi 9 mwaka huu. Adhabu za wachezaji hao ni kwa mujibu wa kifungu cha 27(1)(g) cha Kanuni za FDL.

Klabu ya Villa Squad imepigwa faini ya sh. 150,000 kwa kuchelewa uwanjani kwenye mechi yake dhidi ya Ashanti United wakati Majimaji imepigwa faini ya sh. 200,000 kutokana na washabiki wake kufanya vurugu kwenye mechi dhidi ya Mbeya City iliyochezwa Uwanja wa Majimaji.

Vilevile Msimamizi wa Uwanja wa Majimaji aliyetambulika kwa jina moja la Mapunda aliwatukana waamuzi kwenye mechi hiyo, na suala lake litafikishwa kwenye Kamati ya Nidhamu ya TFF kwa ajili ya hatua za kinidhamu.

Pia uongozi wa Uwanja wa Mafinga unaotumiwa na timu ya daraja la kwanza ya Kurugenzi umetakiwa kuufanyia marekebisho, vinginevyo hautatumika kwa mechi za FDL msimu ujao.

MKUTANO WA WAANDISHI WA HABARI
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kesho (Aprili 11 mwaka huu) litakuwa na Mkutano na Waandishi wa Habari. Mkutano huo utafanyika saa 5 asubuhi kwenye ofisi za TFF.
Boniface Wambura
Ofisa Habari

UEFA KUANZISHA ADHABU MPYA

SHIRIKISHO la Soka barani Ulaya-UEFA limepanga kuanzisha adhabu mpya kali ya kupambana na ubaguzi wa rangi ambap wachezaji watakaokutwa na hatia ya kufanya vitendo hivyo watafungiwa si chini mechi 10. Katika Mkuu wa UEFA Gianni Infantino amesema pia watafunga viwanja kwa muda viwanja ambavyo mashabiki wake watafanya tukio kama hilo kwa mara ya kwanza na kuufunga kabisa kama mashabiki wa timu husika watarudia tukio hilo kwa mara ya pili pamoja na faini ya fedha nyingi. Adhabu hizo mpya ambazo zilizungumziwa katika kikao cha kamati ya utendaji ya UEFA kilichokutana jana kitahusisha mechi zote za mashindano barani Ulaya. Infantino alifafanua kuwa kama mashabiki wa klabu fulani watakutwa na hatia ya kufanya vitendo hivyo basi upande wa uwanja uliohusika na tukio hilo utafungwa lakini kama tatizo ilikijirudia basi mashabiki wote watazuiwa kuingia uwanjani na kutozwa faini itakayofikia dola 65,300.

MCHEZA gofu namba moja duniani, Tiger Woods amesema yuko katika kiwango kizuri tayari kukata ukame wa miaka mitano kupita bila kushinda taji kubwa la Masters wiki hii. Woods ndio anapewa nafasi kubwa ya kunyakuwa zawadi ya Koti ya Bluu toka alipofanya hivyo mwaka 2005 na taji la kwanza kubwa toka mwaka 2008 baada ya kurejea kileleni mwa orodha ya wachezaji bora wa mchezo huo kwa kushinda mataji matatu mwaka huu. Nyota huyo alianguka mpaka katika nafasi ya 58 mwaka 2011 kufuatia kukumbwa na kashfa katika maisha yake binafsi na pia kusumbuliwa na majeruhi. Akihojiwa Woods mwenye umri wa miaka 37 amesema kwasasa anajisikia kurejesha makali yake ya zamani hivyo anategemea kufanya vizuri zaidi mwaka huu.

Monday, April 8, 2013

MECHI SITA KUONEKANA SUPERSPORT ‘LIVE’ SUPER WEEK
Kituo cha televisheni cha SuperSport cha Afrika Kusini kitaonesha moja kwa moja mechi sita za Ligi Kuu ya Vodacom katika Super Week kati ya Aprili 11 na Mei 18 mwaka huu.

Mechi hizo ni kati Azam na African Lyon itakayochezwa Aprili 11 mwaka huu badala ya Aprili 10 mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam. Yanga na Oljoro JKT ambayo sasa itachezwa Aprili 13 mwaka huu badala ya Aprili 10 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Azam na Simba itakayochezwa Aprili 14 mwaka huu badala ya Aprili 13 mwaka huu Uwanja wa Taifa, na mechi kati ya Coastal Union na JKT Ruvu itakayochezwa Aprili 16 mwaka huu badala ya Aprili 10 mwaka huu.

Mechi nyingine ya Super Week itakayochezwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga ni kati ya Mgambo Shooting na Yanga itakayofanyika Aprili 17 mwaka huu badala ya Aprili 13 mwaka huu.

Pia mechi nyingine itakayooneshwa live na SuperSport ni kati ya Yanga na Simba itakayofanyika Mei 18 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kutokana na mechi za Super Week, mechi kati ya Mtibwa Sugar na Oljoro JKT iliyokuwa ichezwe Aprili 13 mwaka huu sasa itachezwa Aprili 17 mwaka huu Uwanja wa Manungu, Turiani mkoani Morogoro.

TFF YATAKA MAELEZO YA MCHEZAJI KUHUSU RUSHWA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemtaka mshambuliaji Nsa Job wa Coastal Union kuwasilisha maelezo yake juu ya madai kuwa alipewa rushwa ya sh. milioni mbili ili asiifunge moja ya timu vigogo vya soka nchini.

Job alikaririwa Aprili 3 mwaka huu na kituo cha redio cha Clouds FM katika kipindi cha Amplifier kuwa alipewa kiasi hicho cha fedha na kiongozi wa timu husika ili asiifunge katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom, lakini alipokea fedha hizo na kuifunga timu hiyo.

Baadaye kiongozi huyo alikuwa akimtaka arejeshe fedha hizo. Pia TFF imekiandikia kituo hicho cha redio kutaka nakala ya kipindi hicho ili pamoja na maelezo ya mshambuliaji huyo vipelekwe katika Kamati ya Nidhamu kwa ajili ya hatua za kinidhamu.

TFF itachukua hatua kali dhidi ya Job iwapo hatawasilisha maelezo yake kuhusiana na suala hilo, na imetaka wadau kutoa ushirikiano ili iweze kupambana kikamilifu na vitendo vya rushwa kwenye mpira wa miguu.

 Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)