Wanandinga wa jangwani Yanga SC wamewasili kisiwani Pemba kuweka kambi ya kujiandaa na mtanange mkali dhidi ya wapinzani wao wa jadi, Simba SC Mei 18, katika dimba la Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
wanajangwani hao watakuwa huko hadi siku moja kabla ya mechi itakaporejea jijini Dar es Salaam.
Pamoja na kuwa Yanga tayari imetwaa ubingwa wa Ligi Kuu, lakini imeipa uzito mkubwa mechi hiyo kwa sababu inataka kulipa kisasi cha kufungwa 5-0 na wapinzani wao hao wa jadi mwaka jana.
Tangu utawala mpya uingia madarakani, uongozi wa Yanga chini ya Mwenyekiti, Alhaj Yussuf Mehboob Manji umekuwa ukiumia kichwa na kipigo cha 5-0 mwaka jana.
Mara kadhaa Manji amewahi kukaririwa akisema kwamba 5-0 zinamuumiza kichwa hasa katika wakati ambao idadi ya mabao katika mechi za timu hiyo ilipungua.
Kihistoria, Simba SC imewahi kuipa Yanga vipigo viwili vitakatifu 6-0 mwaka 1977 na 5-0 mwaka jana, wakati Yanga iliifunga SImba 5-0 mwaka 1969.
Safari hii, Yanga imepania kuweka heshima kwa kuhakikisha inaitwangwa simba kwa kipigo kitakatifu na kuvunja rekodi ya 6-0 ya vipigo hivyo.