Friday, July 26, 2013

BAYERN VS DORTMUND JUMAMOSI

Club ya Bayern Munich na Borussia Dortmund zinataraji kushuka dimba siku Jumamosi katika Mechi ya fungua pazi Msimu mpya kugombea

German Super Cup haya yakiwa kama Marudiano ya Fainali ya Mwezi Mei Uwanjani Wembley ya UEFA CHAMPIONZ LIGI ambayo Bayern walishinda Bao 2-1 na kuweka historia ya kuwa Klabu ya kwanza Nchini Germany kutwaa Trebo, yaani Ubingwa wa Germany, Kombe la Germany na Ubingwa wa Ulaya.
Hata hivyo, Dortmund wamesema wao hawasaki kisasi pale Beki wao anaechezea Germany, Mats Hummels, aliposema: “Hii si kisasi cha Wembley! Ni mtihani mzuri kuonyesha Msimu huu tukoje!”
Kawaida German Super Cup hugombewa na Bingwa na yule Mshindi wa Kombe la Germany lakini kwa vile vyote vilichukuliwa na Bayern Msimu uliopita, Mshindi wa Pili wa Bundesliga, ambae ni Borussia Dortmund aliemaliza Pointi 25 nyuma, ndie atacheza na Bayern Munich.
Sura Mpya
Kila Timu, Bayern Munich na Borussia Dortmund, zitaingia kwenye Mechi hii na sura mpya huku Bayern ikiwa na Kocha mpya Pep Guardiola aliembadili Jupp Heynckes, Thiago Alcantara wa Spain akiwa Bayern kutoka Barcelona na Mario Gotze akiwa pia Bayern kutoka Dortmund.
Dortmund pia wanao wapya ambao ni Viungo Pierre-Emerick Aubameyeng toka St Etienne na Henrikh Mkhitaryan kutoka Shakhtar Donetsk lakini wote hawa wapya huenda wasicheze kutokana na kuwa na maumivu.
Tayari Tiketi zote, 80,654 za Westfalenstadion, kama ilivyo maarufu Signal Iduna Park, zimeshauzwa na Mechi hii itatangazwa Nchi 195 Duniani.

Thursday, July 25, 2013

MESSI AKIRI KUWA MATATIZO YA KIAFYA YA VILANOVA YAMEMUATHIRI

Mshambuliaji nyota wa Club ya Barcelona na timu ya taifa ya argentina,Lionel Messi amekiri kuwa matatizo ya kiafya ya Tito Vilanova yamekuwa pigo kubwa kwao lakini ana uhakika kuwa timu hiyo itafanikiwa kupita katika kipindi hicho kigumu cha kuondoka kwa kocha huyo. Vilanova alitangaza kujiuzulu wiki iliyopita ili aweze kuendelea na matibabu yake ya saratani na Barcelona ikamteua kocha wa zamani wa Newell Old Boys, Gerardo Martino kuchukua nafasi yake. Messi amesema wamesikitishwa kwa kilichotokea kwa Vilanova lakini kikosi chao bado kipo imara na wataendelea kusonga mbele kwa heshima yake. Messi ambaye alicheza dakika 45 katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Bayern Munich jana ambao walichapwa kwa mabao 2-0, amesema kwasasa yuko fiti na majeruhi yaliyokuwa yakimsumbua msimu uliopita yamekwisha.

HIGUAIN NA PEPE REINA WOTE WAJIUNGA NA CLUB YA NAPOILI YA ITALY

Mshambuliaji nyota wa kimataifa wa Argentina, Gonzalo Higuain na golikipa wa kimataifa wa Hispania Pepe Reina wanakaribia kukamilisha uhamisho wao wa kwenda Napoli baada ya kufaulu vipimo vya afya. Rais wa klabu ya Napoli, Aurelio De Laurentiis aliandika katika ukurasa wake wa mtandao wa kimajii wa twitter kuwa wachezaji hao wawili walifaulu vipimo vyao na wanatarajiwa kujiunga na wenzao muda wowote.  
 
Higuain ambaye alikuwa akimendewa na klabu za Arsenal na Juventus, ameripotiwa kuigharimu Napoli euro milioni 37 wakati Reina yeye amejiunga na klabu hiyo kwa mkopo akitokea Liverpool. Mwishoni mwa wiki iliyopita Napoli ilimuuza mshambuliaji wake wa kimataifa wa Uruguay Edinson Cavani kwenda Paris Saint Germain kwa uhamisho ulioweka rekodi wa euro milioni 64.

RODGERS ADAI OFA WALITOA ARSENAL HAILINGANI NA THAMANI YA MCHEZAJI HUYO

KOCHA wa Club ya Liverpool Brendan Rodgers amedai kuwa ofa waliyotoa Arsenal hailingani na thamani aliyonayo mshambuliaji wake Luis Suarez. Liverpool imekataa ofa iliyovunja rekodi ya klabu hiyo ya paundi milioni 40 lakini Suarez anaonekana anataka kuzungumza na timu hiyo yenye maskani yake jijini London. Rodgers amesema kama Arsenal wanamtaka mchezaji huyo wanatakiwa watoe dau ambalo litalingana na thamani yake.  
Kwa maana hiyo Arsenal itatakiwa kuongeza dau zaidi baada ya ofa zake mbili kukataliwa na klabu hiyo. Suarez alionekana kwa mara ya kwanza uwanjani toka alipomng’ata mkono beki wa Chelsea Branislav Ivanovic msimu uliopita wakati alipotokea benchi katika mchezo wa kirafiki walioshinda kwa mabao 2-0 dhidi ya timu ya Melbourne. Suarez alijiunga na Liverpool akitokea klabu ya Ajax Amsterdam ya Uholanzi mwaka 2011 kwa ada ya paundi milioni 22.7.

JAVU ASAINI JANGWANI KUIMARISHA SAFU YA USHAMBULIAJI YA YANGA

Mshambuliaji nyota wa Club ya  Mtibwa Sugar ya Morogoro, Hussein Javu amesaini Mkataba wa miaka miwili kujiunga na Mabi
ngwa hao wa ligi kuu msimu uliopita Yanga SC ambapo hii leo asubuhi ameanza mazoezi kwenye Uwanja wa Sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga SC, Abdallah Bin Kleb amesema kwamba wamemalizana na Javu pamoja na klabu yake, Mtibwa na sasa huyo ni mchezaji mpya wa Jangwani.

Katika habari ambazo tumezinasa mchezaji huyo ameigharimu Yanga SC zaidi ya Sh. Milioni 60 kwa pamoja fedha alizopewa za usajili na ambazo klabu yake ya Mtibwa imelipwa.
Yanga SC imeamua kumsajili Javu kuimarisha safu yake ya ushambuliaji baada ya kuona kocha Mholanzi, Ernie Brandts hajaridhishwa na mshambuliaji kutoka Nigeria, Ogbu Brendan Chukwudi na wakati huo huo, Hamisi Kiiza anataka dau kubwa aendelee kuichezea timu hiyo.
Kiiza amemaliza Mkataba wake Yanga SC na ili kuongeza Mkataba mwingine, viongozi wanashindwa kufika dau lake na sasa wanaamua kumsajili Javu.
Javu ni kati ya washambuliaji wazuri Tanzania kwa sasa, ambaye kwa misimu mitatu amekuwa mwiba dhidi ya vigogo wa soka nchini, Simba na Yanga zinapokutana na timu hiyo ya Manungu. 
Kocha Brandts amevutiwa mno na uwezo wa Javu na kwa ujumla amefurahia ujio wake kwenye mazoezi ya Yanga SC leo.Javu ni mchezaji mwenye uzoefu ambaye amekuwa akiitwa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars tangu enzi za Mbrazil, Marcio Maximo ingawa mbele ya Mdenmark, Kim Poulsen hajawahi kupata nafasi.  
Kusajiliwa kwa Javu, kunaongeza ushindani katika safu ya ushambuliaji ya Yanga SC, kwani sasa inakuwa na watu wanne, wengine ni Jerry Tegete, Didier Kavumbangu, Shaaban Kondo, wakati huo huo hatima ya Mnigeria Chukwudi na Kiiza haijajulikana kama wataachwa au watasajiliwa.
Kwa majira haya ya joto, huyo anakuwa mchezaji wa pili wa Mtibwa kusajiliwa Yanga baada ya beki, Rajab Zahir.
Kwa Mtibwa Sugar ni pigo, kwani katika kikosi chao cha kwanza, huyo anakuwa mchezaji wa tatu kuondoka baada ya Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ aliyesajiliwa Simba SC na Shaaban Kisiga aliyejiondoa kwenye timu, baada ya kutofautiana na kocha Mecky Mexime.  
Wakati huo huo, kiungo Rashid Gumbo anaonekana kutikisa kiberiti baada ya kung’ara akiichezea kwa mkopo timu hiyo akitokea Yanga SC. Gumbo amemaliza Mkataba wake Yanga na sasa ili kuendelea kuichezea Mtibwa, lazima wakae naye mezani.Kama ilivyo kawaida kwa Mtibwa ni si jambo la kushangaza kuuza nyota wake kama Arsenal ya England, hali ambayo imepunguza makali yake katika Ligi Kuu miaka ya karibuni, kwani kila nyota anayeibuka anauzwa. Mtibwa iliibuka vizuri katika soka ya Tanzania ikitwaa ubingwa wa Bara mara mbili mfululizo, 1999 na 2000, miaka mitatu tu tangu ianze kucheza Ligi Kuu.