Thursday, May 23, 2013

TIMU YA TAIFA YA CAMEROON YAPATA KOCHA MPYA.

Timu ya taifa ya Cameroon imefanikiwa kupata kocha mpya  Volker Finke kuwa kocha mkuu wa timu hiyo huku kibarua chake cha kwanza Mjerumani huyo ni kuhakikisha timu hiyo inafuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil. Finke anachukua nafasi ya kocha wa muda wa timu hiyo Jean-Paul Akono ambaye aliwekwa hapo kuziba nafasi ya Denis Lavagne Septemba mwaka jana baada ya Mfaransa huyo kushindwa kuisaidia timu hiyo kufuzu michuano ya Mataifa ya Afrika 2012 na 2013. Kocha huyo mwenye umri wa miaka 65 aliwahi kuifundisha klabu ya SC Freiburg kuanzia mwak 1991 mpaka 2007 na atakuwa anafundisha kikosi cha timu ya taifa kwa mara ya kwanza baada ya kutemwa na timu ya Urawa Red Diamonds ya Japan na timu ya Cologne ya nchini kwake. Katika mechi za kufuzu Kombe la Dunia, Cameroon wako kileleni mwa kundi I wakiwa na alama sita katika mechi tatu walizocheza wakifuatiwa na Libya wenye alama tano, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo-DRC alama nne na Togo alama moja. Kazi yake ya kwanza Finke itakuwa ni kukiongoza kikosi cha timu ya taifa ya nchi hiyo katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Ukraine utakaochezwa jijini Kiev Juni 2 mwaka huu kabla ya kuhamishia nguvu zao katika mechi za kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Togo Juni 9, DRC Juni 16 na Libya Septemba 6 mwaka huu

CLUB YA SANTOS YAKATAA OFA YA PILI YA BARCA

MAKAMU wa rais wa klabu ya Santos ya Brazil, Odilio Rodrigues amedai kwamba wamekataa ofa ya klabu ya Barcelona ya Hispania kutaka kumsajili mshambuliaji wao nyota Neymar kwa mara ya pili. Katika siku za hivi karibuni Barcelona ndiyo pekee wameonyesha nia ya kumhitaji mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Brazil na kuripoti kuwa walitaka kuwapa Santos euro milioni 20 ili waweze kumiliki haki za mchezaji huyo kwa asilimia 55. Wakati mahasimu wao nao Real madrid wakiongeza mbio ya kumfukuzia mshambuliaji huyo, Barcelona walitoa kiasi hicho ili waweze kumaliza suala hilo lakini Rodrigues amesisitiza kuwa hawana haraka ya kumuuza Neymar kwa kiasi kidogo kuliko wanachotaka. Rodrigues alithibitisha kuwa ni kweli walipata ofa ya Barcelona kwa mara ya pili lakini waliikataa kwasababu hawakufikia kiwango walichokuwa wakikihitaji. Neymar katika siku karibu ameweka wazi nia yake ya kubakia Santos mpaka baada ya michuano ya Kombe la Dunia 2014, ingawa uhamisho wa kwenda barani Ulaya katika kipindi hiki cha usajili unaonekana kama unaweza kuwepo.

FA CHADAI KUWA CARROL AJITOA TIMU YA TAIFA KUTOKANA NA MAJERUHI.

CHAMA cha Soka nchini Uingereza {FA} kimedai kuwa mshambuliaji wa kimataifa wa nchi hiyo, Andy Carroll amejitoa katika timu ya taifa kutokana na kuwa majeruhi. Carroll mwenye umri wa miaka 24 amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya kisigino baada ya kocha wa timu ya taifa Roy Hodgson kumuita katika kikosi chake ambacho kitacheza mechi mbili za kimataifa za kirafiki kati ya Ireland Mei 29 na Brazil Juni 2 katika Uwanja wa Maracana jijini Rio de Janeiro. Mshambuliaji huyo wa Liverpool amekuwa akicheza kwa mkopo katika klabu ya West Ham United msimu uliopita huku vyombo vya habari nchini Uingereza vikiripoti kuwa klabu hiyo imekubali kumchukua moja kwa moja kwa ada ya paundi milioni 15. Carroll anaungana na nahodha wa Liverpool Steven Gerrard na kiungo wa Arsenal Jack Wilshere kukosa mechi hizo za kujipima nguvu kabla ya mechi za kufuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014 dhidi ya Moldova na Ukraine Septemba mwaka huu.

KOCHA WA LIVERPOOL RODGERS HANA MPANGO WA KUMUUZA SUAREZ.

BOSI wa  majogoo wa jiji la londo Liverpool Brendan Rodgers amesema hana mpango wa kumuuza mshambuliaji nyota wa klabu hiyo Luis Suarez. Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Uruguay alikosa mechi nne za Liverpool mwishoni mwa msimu huu baada ya kufungiwa mechi 10 kwa kumng’ata beki wa Chelsea Branislav Ivanovic lakini alimaliza katika nafasi ya tatu katika orodha ya wafungaji wa Ligi Kuu nchini Uingereza akiwa na mabao 23. Liverpool haijafuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya toka mwaka 2009 lakini pamoja na vilabu vikubwa kummezea mate Suarez, kocha huyo ana imani kwamba ataweza kumbakisha mchezaji huyo kwa msimu ujao. Rodgers amesema kwasasa wanajipanga kutengeneza kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao na Suarez ni sehemu ya kikosi hicho ingawa amekiri kwamba zipo baadhi ya klabu kubwa zinazomtaka.

GARCIA AMUOMBA RADHI MCHEZAJI NAMBA MOJA TIGER WOODS

MCHEZAJI machachali wa  mchezo wa gofu, Sergio Garcia ameomba radhi kwa kauli yake ambayo inaweza kuonekana kama ya kibaguzi kwenda kwa nyota wa mchezo huo anayeshika namba moja kwa ubora Tiger Woods. Garcia mwenye umri wa miaka 33 aliulizwa kama ataweza kula chakula cha jioni na Woods ili kuzungumzia tofauti zao za hivi karibuni na mchezaji huyo kutania kuwa atamuandalia kuku wa kukaanga nyota huyo. Kuku wa kukaanga ni chakula kinachohusishwa na watu weusi huko Marekani haswa wale wanaotoka kusini mwa nchi hiyo. Garcia aliomba radhi kwa kauli hiyo kama imeeleweka vibaya akidai kuwa hakumaanisha chochote kuhusu ubaguzi wa rangi kwa nyota huyo ambao ambaye asili yake ni mweusi.

MURRAY AJITOA MICHUANO YA WAZI UFARANSA:

MCHEZAJI nyota maarufu wa tenisi kutoka Uingereza Andy Murray amejitoa katika michuano ya wazi ya Ufaransa kutokana na maumivu ya mgongo yaliyopelekea kushindwa kuendelea kucheza katika michuano ya wazi ya Italia. Murray ambaye anashika namba mbili katika orodha za ubora Duniani kwa upande wa wanaume amejitoa katika michuano hiyo baada ya kushauriwa na madaktari wake na anatarajia kurejea tena uwanjani katika michuano ya Wimbledon katikati ya mwezi ujao. Nyota huyo ambaye ni bingwa wa michuano ya wazi ya Marekani amesema umekuwa ni uamuzi mgumu kufanya kwani huwa anapenda kucheza jijini Paris lakini imekuwa nje ya uwezo wake kwasababu ya ushauri wa kiafya aliopewa. Murray aliwaomba radhi waandaaji wa michuano hiyo na kuwashukuru mashabiki wake kwa kumtumia ujumbe wa kumuunga mkono na sasa kazi kubwa aliyokuwa nayo ni kuhakikisha anapona na kurejea haraka uwanjani.

Wednesday, May 22, 2013

MWAMUZI WA AFRIKA KUSINI KUICHEZESHA STARS MOROCCO.


Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limemteua mwamuzi kutoka Afrika Kusini kuchezesha mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia, Kanda ya Afrika kati ya Tanzania (Taifa Stars) na wenyeji Morocco (Lions of the Atlas).

Mechi hiyo ya kundi C itachezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech, Morocco kwenye Uwanja wa Grand kuanzia saa 3 kamili usiku kwa saa za Morocco. Mwamuzi atakayechezesha mechi hiyo ni Fraser Daniel Bennett.

Bennett atasaidiwa na Thusi Zakhele Siwela pia wa Afrika Kusini, wakati mwamuzi msaidizi namba mbili atakuwa ni Marwa Range kutoka Kenya. Mwamuzi wa akiba (fourth official) ni Lwandile Mfiki wa Afrika Kusini.

Kamishna wa mechi hiyo ni Robert Mangollo-M’voulou wa Gabon wakati mtathimini wa waamuzi (referee assessor) ni Charles Masembe kutoka Uganda.

Taifa Stars ambayo iko chini ya Kocha Kim Poulsen, na ikidhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager tayari iko kambini katika hoteli ya Tansoma ikiendelea kujinoa kwa ajili ya mechi hiyo ambapo kabla itajipima na Sudan (Nile Crocodiles) Juni 2 mwaka huu jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Ratiba ya mazoezi kwa timu hiyo ni kama ifuatavyo;

Mei 22                 Saa 10 jioni                             Uwanja wa Karume
Mei 23                 Saa 1 asubuhi na Saa 10 jioni   Uwanja wa Karume
Mei 23                 Saa 10 jioni                             Uwanja wa Karume


Mei 25                 Saa 1 asubuhi na Saa 10 jioni     Uwanja wa Karume
Mei 26                 Saa 3 asubuhi                            Uwanja wa Karume


MSIMAMO WA KUNDI C:


                     P W D L GF GA Pts
Ivory Coast 3 2 1 0 7 2 7
Tanzania 3 2 0 1 5 4 6
Morocco 3 0 2 1 4 6 2
Gambia 3 0 1 2 2 6 1


REKODI YA KIM POULSEN STARS
Mei 26, 2012
Tanzania 0 – 0 Malawi (Kirafiki)
Juni 2, 2012
Ivory Coast 2 – 0 Tanzania (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 10, 2012
Tanzania 2 – 1 Gambia (Kufuzu Kombe la Dunia)
Juni 17, 2012
Msumbiji 1 – 1 Tanzania  (Tanzania ilitolewa
kwa penalti kufuzu Mataifa ya Afrika)
Agosti 15, 2012
Botswana 3 – 3 Tanzania (Kirafiki)
Novemba 14, 2012
Tanzania 1-0 Kenya (Kirafiki)
Desemba 22, 2012
Tanzania 1-0 Zambia (Kirafiki)
Januari 11, 2013
Tanzania 1-2 Ethiopia (Kirafiki)
Februari 6, 2013
Tanzania 1-0 Cameroon (Kirafiki)
Machi 22, 2013
Tanzania 3-1 Morocco (Kufuzu Kombe la Dunia)



MKUTANO WA WAANDISHI WA HABARI
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga atakuwa na mkutano na waandishi wa habari. Mkutano huo utafanyika kesho (Mei 23 mwaka huu) saa 5 kamili asubuhi kwenye ukumbi wa mikutano wa TFF.



Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)