Friday, August 16, 2013

MOURINHO ASEMA NATAKA KUWEKA POA FAMILIA YA WANACHELSEA

Meneja wa Chelsea, Jose Mourinho amesema  lengo kuu anataka kurudisha upya familia ya wadau wa Chelsea ambayo ilivunjika baada ya kocha aliyeondoka Rafa Benitez kumrithi kocha kipenzi cha mashabiki Roberto Di Matteo na kusababisha tofauti kwa mashabiki wa klabu hiyo.
Chelsea waliingia katika vita ya wenyewe kwa wenyewe baada ya kumfukuza kocha aliyewapa ubingwa wa ligi ya mabingwa barani Ulaya, na hata baada ya Benitez kushinda kombe la Uropa haikumnusuru kufungashiwa virago.
Ambapo mmiliki Roman Abramovich alimgeukia tena kwa mara ya pili  Mourinho majira haya ya kiangazi na amefanikiwa kumrejesha.
Kocha huyo mwenye Umri wa miaka 50, raia wa Ureno aliliambia gazeti la The Sun: “Nawataka kuwa nasi kama familia ya Chelsea-familia ambayo kwa muda fulani mwaka jana ilionekana kuvunjika”.

SUAREZ ARUDI NYUMBANI ANFIELD BAADA YA MISUKOSUKO YA HAPA NA PALE YA KUTAKA KUONDOKA"

Mshambuliaji nyota Luis Suárez leo amerudi kikosini huko Anfield na kuanza Mazoezi tena pamoja na Kikosi cha Kwanza cha Timu ya Liverpool baada ya kuzuiwa kufanya hivyo na Meneja Brendan Rodgers kwa kuishambulia Klabu kwa madai ya kuvunja ahadi ya kumruhusu ahame ikiwa haitafuzu kucheza UEFA CHAMPIONZ LIGI Msimu huu.
Jumanne iliyopita Suarez alilazimishwa kufanya Mazoezi peke yake na kutakiwa kuiomba Klabu radhi kwa kauli zake na inaaminika Mchezaji huyo ametii amri hiyo na ndio maana amerudishwa tena Mazoezini kwenye Kikosi cha Kwanza.
Suarez amekuwa akisinikiza kuihama Liverpool na Arsenal ilishatoa Ofa ya Pauni 40,000,001 kumnunua lakini Liverpool imekataa na kusisitiza Mchezaji huyo hauzwi.
Msimamo huo ulisisitizwa zaidi na Mmiliki mkuu wa Liverpool kutoka Marekani, John W Henry, ambae Wiki iliyopita alitamka Suarez hatauzwa kwa Arsenal au kwa Klabu yeyote Ulaya.
Kwa sasa Suarez yupo kwenye Kifungo cha Mechi 10 alichopewa mwishoni mwa Msimu uliokwisha Mwezi Mei kwa kumng’ata meno Beki wa Chelsea Branislav Ivanovic kwenye Mechi na tayari ameshatumuikia Mechi 4 na bado 6.
Wakati huo huo, Liverpool imefanikiwa kukubaliana na Klabu ya Spain, Valencia, ili kumchukua Beki wao wa kushoto Aly Cissokho kwa Mkopo wa Msimu mmoja.
Meneja wa Liverpool Brendan Rodgers alikuwa akisaka Mchezaji wa pozisheni hiyo ili kuleta ushindani kwa Beki wake José Enrique na waliwahi kuwawania Lorenzo Melgarejo wa Benfica na Guilherme Siqueira wa Granada ili kujaza Nafasi hiyo.

KAMATI YASHERIA NA HADHI ZA WACHEZAJI YA TFF YATOA MAAMUZI KUHUSU NGASA"


KAMATI ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imepitia usajili wa wachezaji wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom na kumuidhinisha Mrisho Ngasa kuchezea timu ya Yanga baada ya kukamilisha usajili wake.
Hata hivyo, Kamati hiyo chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa imebaini kuwa Ngasa alisaini mkataba mwingine Simba (katika kipindi ambacho alikuwa na mkataba na Azam) ambapo anatakiwa kurejesha fedha alizopokea (sh. milioni 30) pamoja na fidia ya asilimia 50 (sh. milioni 15) ya fedha hizo kwa Simba.
Kamati pia imemfungia mechi sita za mashindano (kuanzia mechi ya Ngao ya Jamii), na anatakiwa awe amelipa fedha hizo ndani ya kipindi hicho cha kukosa mechi hizo. Akishindwa, hataruhusiwa kucheza hadi atakapolipa fedha hizo.

Vilevile Kamati imepitia pingamizi zote zilizowasilishwa kuhusu usajili wa wachezaji, kukatiza mikataba ya wachezaji na kuzitaka klabu husika ziwe zimetatua masuala hayo hadi Alhamisi (Agosti 22 mwaka huu).
Kwa upande wa wachezaji wa kigeni, Kamati imeagiza wasiruhusiwe kucheza hadi watakapopata Hati za Uhamisho wa Kimataifa (ITC) pamoja na vibali vya kufanya kazi nchini (work permits).
Kamati hiyo itakutana tena Ijumaa (Agosti 23 mwaka huu) ili kupata ripoti za pingamizi ilizoagiza ziwe zimefanyiwa kazi hadi Agosti 22 mwaka huu na kutoa uamuzi kwa pande ambazo hazikuafikiana.
Wakati huo huo: Kamati ya TFF kwa kuzingatia mamlaka iliyonayo katika kifungu cha 10(6) cha Kanuni za Uchaguzi za TFF inasogeza mbele tarehe ya uchaguzi wa TFF kutoka Oktoba 20 mpaka Oktoba 26 na 27 mwaka huu.
Sababu za kusogeza mbele uchaguzi ni kutokana na ukweli kuwa Oktoba 20 mwaka huu uongozi wa TFF utakuwa na shughuli nyingi za maandalizi ya mechi ya Simba na Yanga, na hivyo haitawezekana kusimamia shughuli za Mkutano Mkuu wa Uchaguzi kwa wakati mmoja na mchezo huo.
Siku ya mwisho ya kampeni itakuwa Oktoba 25 mwaka huu. Ukiondoa  mabadiliko hayo ya tarehe ya uchaguzi wa viongozi wa TFF, ratiba ya mchakato wa uchaguzi na itabaki kama ilivyotangazwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF katika mkutano wake na waandishi wa habari Agosti 24 mwaka huu.
Pia Kamati imeamua kuwa uchaguzi wa Bodi ya Ligi utabakia kuwa Oktoba 18 mwaka huu kama ilivyopangwa awali.
Kamati imesema inaamini wahusika wote watapokea vizuri mabadiliko hayo na inasikitika kwa usumbufu utakaosababishwa na mabadiliko hayo.




KAMATI YA UCHAGUZI KUJADILI SIMBA, YANGA

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemwandikia Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ili kufanya uamuzi wenye manufaa kwa washabiki wa mpira wa miguu baada ya tarehe ya uchaguzi aliyotangaza kuingilia na mechi ya watani wa jadi (Simba na Yanga) ya Ligi Kuu ya Vodacom.
Sekretarieti ya TFF imepokea maoni kutoka kwa wapenzi mbalimbali wa mpira wa miguu wakiomba matukio hayo mawili (Uchaguzi wa TFF na mechi ya Simba na Yanga) yafanyike katika siku tofauti.
Wakati Kamati ya Uchaguzi inatangaza uchaguzi kufanyika Oktoba 20 mwaka huu tayari ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom ilikuwa imeshatoka, na ikionesha kuwa timu ambazo zina historia ya kipekee katika mpira wa miguu zitacheza siku hiyo.
Sekretarieti imelazimika kumwandikia Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi kwa vile yeye na kamati yake ndiye wenye mamlaka ya kuitisha Mkutano wa Uchaguzi. Huko nyuma TFF imeshafanya mikutano huku kukiwa na mechi za timu ya Taifa (Taifa Stars), jambo ambalo liliwezekana kutokana na mikutano hiyo kuwa na ajenda moja tu.
Tayari Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Hamidu Mbwezeleni ameitisha kikao cha kamati yake kujadili barua hiyo ya sekretarieti.
COCA COLA YATOA MIPIRA 100, FULANA 800
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa shukrani kwa kampuni ya Coca Cola kwa kukabidhi fulana 800 na mipira 100 kwa ajili ya ngazi ya mashindano ya vijana wenye umri chini ya miaka 15 ngazi ya mikoa yanayoanza Septemba Mosi mwaka huu.
Coca Cola ndiyo inayodhamini mashindano hayo yaliyoanzia ngazi ya wilaya ambapo mwaka huu yatachezwa kwa kanda na baadaye fainali itakayochezwa kuanzia Septemba 7-14 mwaka huu jijini Dar es Salaam ikishirikisha mikoa 16 itakayokuwa imefanya vizuri katika ngazi ya kanda.
Kila mkoa utapata fulana 25 na mipira mitatu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya timu zao kwa ajili ya michuano hiyo ngazi ya kanda itakayomazika Septemba 6 mwaka huu.
Kanda hizo ni Mwanza itakayokuwa na timu za mikoa ya Geita, Kagera, Kigoma, Mara, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Tabora. Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara na Singida inaunda Kanda ya Arusha.
Zanzibar itakuwa na Kaskazini Pemba, Kusini Pemba na mikoa miwili ya Unguja wakati Kanda ya Dar es Salaam ina Ilala, Kinondoni, Lindi, Mtwara, Temeke na mkoa mmoja wa Unguja.
Kanda ya Mbeya inaundwa na Iringa, Katavi, Mbeya, Njombe, Rukwa na Ruvuma wakati Dodoma, Morogoro, Pwani na Tanga zinaunda Kanda ya Morogoro.
Mwanza itatoa timu nne kucheza hatua ya fainali wakati kanda nyingine za Arusha timu mbili, Zanzibar (2), Mbeya (3) na Kanda ya Morogoro itaingiza timu mbili.
Wakati huo huo, semina ya makocha 32 wa timu za mikoa zitakazoshiriki michuano ya U15 FIFA Copa Coca-Cola iliyokuwa ikiendeshwa na mkufunzi Govinder Thondoo kutoka Mauritius inafungwa leo (Agosti 16 mwaka huu) saa 9 alasiri kwenye ukumbi wa Msimbazi Center, Dar es Salaam.

RAMBIRAMBI MSIBA WA MWANDISHI GRACEMO BAMBAZA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha aliyekuwa mwandishi wa habari za michezo wa Radio ABM ya Dodoma, Gracemo Bambaza kilichotokea Agosti 14 mwaka huu katika Hospitali ya Ocean Road, Dar es Salaam.
Msiba huo ni mkubwa katika sekta ya habari na mpira wa miguu kwani Bambaza kwa kipindi chote akiwa mwandishi alikuwa akifanya kazi nasi, hivyo mchango wake katika mpira wa miguu tutaukumbuka daima.
Bambaza aliyezaliwa mwaka 1973 na ambaye pia aliwahi kufanya kazi katika vituo vya redio vya Wapo cha Dar es Salaam na Pride cha Mtwara amesafirishwa jana (Agosti 15 mwaka huu) kwenda Karagwe mkoani Kagera kwa ajili ya mazishi.
TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Bambaza, ABM Radio na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.
Mungu aiweke roho ya marehemu Bambaza mahali pema peponi. Amina 

TIKETI MECHI YA YANGA, AZAM KUUZWA ASUBUHI
Tiketi kwa ajili ya mechi ya Ngao ya Jamii kati ya Yanga na Azam itakayochezwa kesho (Agosti 17 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam zitaanza kuuzwa saa 3 asubuhi.
Vituo vitakavyouza tiketi hizo Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala na BMM Barber Shop iliyoko Sinza Madukani.
Katika vituo hivyo tiketi zitauzwa katika magari maalumu. Magari yote yanayouza tiketi yatahamia uwanjani saa 7 kamili mchana.
Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 7,000 kwa viti vya rangi ya kijani na bluu wakati viti vya rangi ya chungwa ni sh. 10,000. Watakaiongia viti vya VIP C watalipa sh. 15,000, viti vya VIP B ni sh. 20,000 wakati VIP A watalipa sh. 30,000.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Thursday, August 15, 2013

KANU ANAAMINI NCHI YAKE NIGERIA INA UWEZO MKUBWA"

Mshambuliaji wa zamani Arsenal, Nwankwo Kanu, anaamini Nchi yake Nigeria inao uwezo wa kufuzu kucheza Fainali za Kombe la Dunia huko Brazil Mwaka 2014 na pia kufanya vyema.
Kanu amesema lengo lao ni kutwaa Ubingwa wa Dunia Mwaka 2014 kwa ajili ya Afrika.
Hadi leo hakuna Nchi hata moja ya Afrika iliyoweza kutinga Nusu Fainali za Kombe la Dunia na katika Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka 2010 huko Nchini Afrika Kusini, Ghana ilikosa kidogo kuwa Nchi ya kwanza kuingia Nusu Fainali ilipofanyiwa ukatili na Luis Suarez pamoja na Uruguay yake.
Kanu, aliewahi kuzichezea Klabu za Portsmouth, Arsenal, Inter Milan na Ajax, anaamini Nigeria, ambao ndio Mabingwa wa Afrika, wanayo Timu imara na Benchi la Makocha mahiri ambalo linaweza kuiwezesha Nchi hiyo kufuzu kwenda Brazil na kuonyesha maajabu.
Kanu, mwenye Miaka 37, alisema: “Ni wazi tutafika Fainali za Kombe la Dunia Mwakani na tunataka kutwaa Kombe kwa ajili ya Afrika. Bado tuna Mechi na Malawi na tuko tayari na tutafanya kila tuwezalo.”
Baada ya kutwaa Ubingwa wa Afrika Mwezi Januari, Nigeria waliiwakilisha Afrika kwenye Mashindano ya FIFA ya Kombe la Mabara huko Brazil Mwezi Juni lakini waliishia hatua ya Makundi tu waliposhindwa kufuzu toka Kundi lao lililokuwa na Timu za Spain, Uruguay na Tahiti.
Ili kufika Fainali za Kombe la Dunia huko Brazil Mwaka 2014, Nigeria wanahitaji kutofungwa Mechi ya Nyumbani ya mwisho ya Kundi lao dhidi ya Malawi hapo Septemba 7 na kisha kuifunga Timu watakayopangiwa kwenye Raundi ya Mwisho ya Mtoano ambapo zitachezwa Mechi mbili za Nyumbani na Ugenini.
Wakati huo huo, hapo Jana huko Moses Mabhida Stadium Nchini Afrika Kusini, Nigeria waliwafunga Afrika Kusini Bao 2-0 na kutwaa Taji la Nelson Mandela Challenge huku Bao zote zikifungwa Kipindi cha Pili na Uche Nwofor alietokea Benchi.

YANGA, AZAM KUVAANA NGAO YA JAMII J’MOSI

Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom, Yanga na makamu bingwa Azam wanavaana keshokutwa (Jumamosi) kwenye mechi ya Ngao ya Jamii (Community Shield) kuashiria uzinduzi wa msimu mpya wa 2013/2014.

Mechi hiyo inayotarajiwa kuwa kivutio kwa wapenzi wa mpira wa miguu nchini itachezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10.30 jioni ambapo mshindi atakabidhiwa ngao.


Iwapo dakika 90 za mechi hiyo hazitatoa mshindi, timu hizo zitatenganishwa kwa mikwaju ya penalti huku asilimia 10 ya mapato ya mechi hiyo yakienda kwa kituo cha kulelea watoto cha SOS.


Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 7,000 kwa viti vya rangi ya kijani na bluu wakati viti vya rangi ya chungwa ni sh. 10,000. Watakaiongia viti vya VIP C watalipa sh. 15,000, viti vya VIP B ni sh. 20,000 wakati VIP A watalipa sh. 30,000.

LIGI DARAJA LA KWANZA KUANZA SEPT 14

Michuano ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inayoshirikisha timu 24 zilizogawanywa katika makundi matatu msimu huu (2013/2014) itaanza kutimua vumbi Septemba 14 mwaka huu.


Kila timu itakayoongoza kundi lake katika ligi itakayochezwa kwa mikondo miwili (nyumbani na ugenini) ndiyo itakayopanda daraja kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu wa 2014/2015.


Mechi za ufunguzi kwa kundi A zitakuwa kati ya Tessema vs Green Warriors (Uwanja wa Karume, Dar es Salaam) wakati Septemba 15 mwaka huu ni Transit Camp vs Polisi Dar (Uwanja wa Mabatini, Pwani), Ndanda vs Friends Rangers (Uwanja wa Nangwanda, Mtwara) wakati Villa Squad vs African Lyon itachezwa Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.


Kundi B ni Burkina Faso vs Polisi Moro (Uwanja wa Jamhuri, Morogoro), Mkamba Rangers vs Lipuli (Uwanja wa CCM Mkamba, Morogoro), Majimaji vs Mlale JKT (Uwanja wa Majimaji, Songea) wakati Septemba 15 mwaka huu Kimondo SC vs Kurugenzi (Uwanja wa Sokoine, Mbeya).


Mechi za ufunguzi kundi C ni Polisi Mara vs Polisi Dodoma (Uwanja wa Karume, Musoma), Kanembwa JKT vs Polisi Tabora (Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma), Stand United vs Mwadui (Uwanja wa Kambarage, Shinyanga), na Pamba vs Toto Africans (Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza).


Mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo utamalizika Oktoba 26 mwaka huu wakati wa pili utamalizika Machi 22 mwakani. (Ratiba imeambatanishwa)


Boniface Wambura

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

RIBERY AWAHI KUFIKIRIA KUICHEZEA BARCELONA PAMOJA NA REAL MADRID"

Winga wa club ya Bayern Munich, Franck Ribery amekiri kuwahi kufikiria kuihama klabu hiyo na kwenda Barcelona katika kipindi cha majira ya kiangazi mwaka 2009 lakini aliamua kuheshimu mkataba wake na kubakia. Winga huyo wa kimataifa wa Ufaransa pia alikuwa akihusishwa na kutaka kusajiliwa na Real Madrid miaka michache iliyopita lakini sasa ameweka wazi kuwa Madrid sio klabu pekee iliyokuwa ikimhitaji nchini Hispania. 

Ribery amedai kuwa mchezaji mwenzake wa timu ya taifa ya Ufaransa, Eric Abidal ambaye alikuwa akicheza chini ya Pep Guardiola akiwa Barcelona alimfuata na kumwambia suala hilo katika msimu wa 2008-2009. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 30 alikiri kufikiria kujiunga na klabu hiyo kwa kipindi hicho kwasababu walikuwa na kikosi bora duniani. Ribery aliendelea kudai kuwa alikuwa katika kipindi kigumu kufanya uchaguzi lakini kwasababu ya umuhimu wa Karl-Heinz Rummenigge na Uli Hoeness ambaye ndiye rais wa klabu hiyo kwake aliamua kuheshimu mkataba wake na kutulia.

Wednesday, August 14, 2013

SUAREZ AJA NA MTAZAMO MPYA KUHUSU KUBAKIA LIVERPOOL

Mshambuliaji mahiri wa club ya Liverpool, Luis Suarez amebadili mawazo kuhusu mustakabali wake na kusisitiza kuwa ameamua kubakia Anfield. Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Uruguay amekuwa akitaka kuondoka Uingereza kutokana na kuchoshwa na vyombo vya habari vya nchi hiyo lakini Liverpool walikuwa hawako tayari kumuachia nyota huyo. Arsenal ambao ushiriki wao katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya ulionyesha kumvutia Suarez, walijitahidi kujaribu kumsajili nyota huyo mwenye umri wa miaka 26 kwa kutoa ofa ya paundi milioni 42 ambayo ingevunja rekodi yao ya usajili lakini walikataliwa. Akihojiwa jijini Tokyo akiwa katika majukumu ya timu yake ya taifa, Suarez amebainisha kuwa ameamua kubakia kwa ajili ya mashabiki wa klabu hiyo ambao wameonyesha mapenzi makubwa kwake.

YANGA YAINGIA KAMBINI KUJINOA DHIDI YA AZAM NGAO YA JAMII



MABINGWA wa ligi kuu msimu uliopita  YANGA SC wameingia kambini makao makuu ya klabu yao, Jangwani, Dar es Salaam maarufu kama Jangwani City kujiandaa na mchezo wa kuwania Ngao ya Jamii dhidi ya Azam FC Jumamosi, Uwanja wa Taifa, Jijini.
Wakati mabingwa hao wa Ligi Kuu, wakiingia kambini Jangwani, wapinzani wao Azam FC waliorejea jana kutoka Afrika Kusini walipoweka kambi ya takriban wiki mbili, wamefikia kwenye makao yao makuu, Azam Complex, Chamazi, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Mchezo huo wa kuashiria kufungua pazia la msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara umeteka hisia za wengi na kila timu inaonekana kupania kushinda ili kuwasha taa za kijani kuelekea mbio za ubingwa.
Yanga iliifunga Azam FC katika mechi zote tatu za msimu uliopita walizokutana, hivyo kulipa kisasi cha kufungwa na timu hiyo ya Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa mara nne msimu uliotangulia katika mashindano yote waliyokutana.  
Katika kujiandaa na msimu, Yanga SC walicheza mechi saba na kushinda tatu, kufungwa moja na sare tatu.
Walizifunga Mtibwa Sugar 3-1, SC Villa ya Uganda 4-1 na 3Pillars ya Nigeria 1-0, na kutoa sare ya 1-1 na Express, 2-2 na URA zote za Uganda na 0-0 na Rhino FC mjini Tabora, wakati walifungwa 2-1 na Express ya mjini Shinyanga.
Kwa upande wa washindi wa pili wa Ligi Kuu, Azam kabla ya kwenda Afrika Kusini walicheza mechi nne na kushinda tatu, 1-0 na komabini ya JKT, 4-0 na African Lyon na 5-1 Ashanti United. Azam pia ilicheza mechi tatu na kikosi chake cha pili, Azam Akademi na kushinda zote, 1-0 mara mbili na 2-1 mara moja.
Na ikiwa Afrika Kusini, ilicheza mechi nne na kufungwa tatu na kushinda moja- ilifungwa 3-0 na Kaizer Chiefs, 2-1 na Orlando Pirates na 1-0 na Moroka Swallows, wakati yenyewe ilishinda 1-0 dhidi ya Mamelodi Sundowns.