Saturday, November 22, 2014

CAF YAMTEUA SAM MPENZU KUTOKA TZ MCHUZO WA AFCON 2015.

Shirikisho la Soka Africa (Caf) limemteua mwamuzi kutoka nchini Tanzania, Samwel Mpenzu kushiriki kwenye mchujo wa kuwapata waamuzi watakaochezesha michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon 2015) inayotarajiwa kufanyika mwakani nchini Equatorial Guinea.

Iwapo Mpenzu atafuzu mchujo huo, atakuwa ni Mtanzania wa tatu kuchezesha michuano mikubwa kama hiyo barani Afrika, waamuzi wengine waliowahi kuchezesha ni Omar Abdulkadir na Ferdinand Chacha aliyechezesha Afcon (U-21).

Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Salumu Umande, amesema kuwa wameshapokea taarifa hizo za kuteuliwa kwa Mpenzu na tayari ameshawasili nchini Misri kwa ajili ya mchujo huo ambao unatarajiwa kufanyika kati ya leo (Jumamosi) na kesho.

Amesema kuwa iwapo atafanikiwa kufuzu kwenye mchujo huo, atapata nafasi ya moja kwa moja ya kuchezesha fainali hizo, kitu ambacho kitakuwa ni hatua kubwa kwa waamuzi wa Tanzania kwani kwa miaka mingi hakuna mwamuzi hata mmoja kutoka Tanzania aliyepata nafasi hiyo.