Friday, June 28, 2013

WAWILI WACHAGULIWA KITUO CHA VIPAJI ASPIRE

Wachezaji wawili kutoka Tanzania wamechaguliwa miongoni mwa 50 waliofanyiwa majaribio nchini Uganda kwa ajili ya kuingia katika kituo cha kuendeleza vipaji (centre of excellence) kilichoko Doha nchini Qatar kupitia mpango wa kukuza vipaji wa Aspire Football Dream.
Abdulrasul Tahir Bitebo (15) ambaye ni mshambuliaji kutoka Kituo cha Uwanja wa Karume, na Martin Omela Tangazi (14) ambaye ni beki kutoka Kituo cha Ukonga ndiyo waliochaguliwa kutoka Tanzania kuingia katika kituo ambapo watakaa kwa mwezi mmoja kabla ya kusaini mkataba rasmi wa kuendelezwa.

Wachezaji wengine walikuwa wakitoka katika nchi za Uganda na Kenya. Mchezaji mwingine aliyefuzu katika nafasi tatu zilizokuwepo ni kutoka nchini Kenya.

Mpango wa Aspire Football Dream unafadhiliwa na Mtoto wa Mfalme wa Qatar katika nchi 16 duniani, na kwa hapa nchini uko chini ya Idara ya Ufundi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

TFF ina jumla ya vituo 14 vya kuendeleza vipaji kupitia mpango huo wa Aspire Football Dream. Vituo hivyo ni Karume, Kigamboni, Tandika, Kawe, Ukonga, Kitunda, Mbagala, Magomeni, Makongo, na Tabata vilivyo katika Mkoa wa Dar es Salaam. Vingine ni Bagamoyo kilichopo mkoani Pwani, Morogoro, Arusha na Moshi mkoani Kilimanjaro.

Kituo kingine cha kuendeleza vipaji (centre of excellence) cha Aspire kipo Dakar nchini Senegal.

TFF KUENDESHA KOZI SITA KATI YA JULAI- SEPTEMBA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) litaendesha kozi sita tofauti za mpira wa miguu kati ya Julai na Septemba mwaka huu.

Kozi hizo ni FIFA 11 For Health itakayofanyika Hombolo mkoani Dodoma kuanzia Julai 8 hadi 19 mwaka huu. Julai 6 hadi 15 mwaka huu kutakuwa na kozi ya mpira wa miguu wa ufukweni (Beach Soccer) itakayofanyika jijini Dar es Salaam.

Waamuzi wa FIFA nao watakuwa na kozi itakayofanyika kati ya Agosti 22 hadi 26 mwaka huu jijini Dar es Salaam wakati kozi ya ukocha kwa ajili ya Copa Coca-Cola itafanyika jijini Dar es Salaam kati ya Agosti 12 na 17 mwaka huu.

Vilevile kutakuwa na kozi ya mpango wa grassroots unaolenga wachezaji mpira wa miguu (wasichana na wavulana) wenye umri kuanzia miaka 6-12 itafanyika kuanzia Septemba 9 hadi 13 mwaka huu jijini Dar es Salaam wakati tamasha (festival) la grassroots litafanyika Uwanja wa Karume, Septemba 14 mwaka huu.

RCL KUKAMILISHA HATUA YA NNE JUMAPILI
Mechi za marudiano za hatua ya nne ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) zitachezwa Jumapili (Juni 30 mwaka huu) kwenye viwanja vya Sokoine jijini Mbeya, na Kambarage mjini Shinyanga.

Friends Rangers ya Dar es Salaam ambayo katika mechi ya kwanza ilifungwa nyumbani mabao 3-0 itakuwa mgeni wa Stand United FC mjini Shinyanga wakati Kimondo SC itaikaribisha Polisi Jamii ya Mara jijini Mbeya. Katika mechi ya kwanza timu hizo zilitoka sare ya mabao 2-2.

Hatua ya mwisho ya RCL itachezwa Julai 3 mwaka huu kwa mechi za kwanza wakati zile za marudiano zitafanyika Julai 7 mwaka huu. Timu tatu za kwanza zitapanda daraja kucheza Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu ujao.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

TENGA ASEMA MKUTANO UPO PALEPALE"-MKUU WA TFF

TFF_LOGO12SHIRIKISHO la Soka Tanzania, TFF, limethibitisha kuwa Mkutano Mkuu wao uliopangwa kufanyika Julai 13 utaendelea licha ya kuwa Siku hiyo hiyo Tanzania inacheza Mechi ya kwanza ya Mchujo ya CHAN dhidi ya Uganda Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.
Wadau wengi wamekuwa wakihoji kufanyika kwa Mkutano huo wakati Nchi inakabiliwa na Mechi muhimu Siku hiyo hiyo huku wengine wakidiriki kudai kuna walakini ndani yake.
Lakini Rais wa TFF, Leodegar Tenga, amefafanua kuwa vitu hivyo viwili haviwezi kuleta mgongano kwani Mechi itachezwa kwa Dakika 90 na Mkutano Mkuu umepangwa kuwa wa Siku mbili.
Tenga alisema: “Hamna njama zozote. Vitu hivyo viwili vitaendelea kama ilivyopangwa.”
Akifafanua, Tenga alisema Wajumbe wa Mkutano Mkuu wamezoea kujadili Ajenda hadi 12 katika Siku moja lakini safari hii Ajenda ni moja tu na imepangiwa Siku mbili.
Ajenda ya Mkutano Mkuu huo ni kujadili na kupitisha Mabadiliko ya Katiba ili kuruhusu Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho hilo ufanyike kama ilivyoagizwa na FIFA.
Awali Uchaguzi ulikuwa ufanyike hapo Februari 24 lakini ukatokea mgongano mkubwa baada ya baadhi ya Wagombea kufutwa na pia madai kuwa Katiba ilibadilishwa bila kufuata taratibu.
Akifafanua zaidi, Tenga alisema upo uwezekano mkubwa kwa Wajumbe wa Mkutano Mkuu kumaliza Kikao chao kabla hata Mechi kuchezwa.
Katika Uchaguzi wa awali Tenga hakuwa Mgombea wa nafasi yake.

Thursday, June 27, 2013

FEDERER ASEMA BADO ATAENDELEA KUCHEZA MCHEZO HUO".

Mchezaji tenesi mahiri wa Switzerland, Roger Federer amesisitiza kuwa bado ataendelea kucheza mchezo huo kwa miaka mingi ijayo pamoja na kutolewa mapema katika michuano ya Wimbledon jana. Nyota huyo ambaye anashika namba tatu katika orodha za ubora duniani amesema hana hofu yoyote pamoja na kutolewa na Sergiy Stakhovisky wa Ukraine katika mzunguko wa pili wa michuano hiyo. Katika mchezo huo Federer aliburuzwa kwa kufungwa 6-7 7-6 7-5 7-6 na Stakhovsky anayeshika namba 116 katika orodha za ubora duniani. Baadhi ya wadau wa mchezo huo wamekuwa wakihoji kiwango cha Federer mwenye umri wa miaka 31 na kudai kuwa amekwisha lakini mwenye amesisitiza kuwa bado yuko fiti na ataendelea kucheza kwa miaka kadhaa ijayo. Kwa upande wa wanawake mwanadada nyota anayeshika namba mbili kwa ubora kwa upande wanawake Maria Sharapova wa Urusi naye aliyaaga mashindano hayo baada ya kukubali kipigo cha 6-3 6-4 kutoka kwa Michelle Larcher de Brito wa Ureno anayeshika namba 131 katika orodha hizo.

SCOLARI AMEKIRI KUWA TIMUYA BRAZIL BADO HAIKO FITI-DUNIA

KOCHA wa timu ya taifa ya Brazil, Luis Felipe Scolari amekiri kuwa kikosi chake bado hakiwezi kuanza kuweka matumaini ya kutwaa kombe lao la sita la Kombe la Dunia mwaka ujao lakini wamebakisha mechi moja kunyakuwa taji lao la tatu la Kombe la Shirikisho baada ya kuiengua Uruguay katika hatua ya nusu fainali. Scolari amesema anafikiri kikosi hicho kimefikia mahali pazuri lakini bado kuna vitu vingi vya kufanyia marekebisho mpaka kikamilike kwa ajili ya michuano ya Kombe la Dunia mwakani. Kocha huyo aliendelea kudai kuwa kwasasa wanahamishia nguvu zao katika mchezo wa fainali na baada ya hapo wataangalia mapungufu yalijitokeza ili kuhakikisha wanakuwa na kikosi imara kitakachoweza kulibakisha Kombe la Dunia nyumbani. Brazil kwasasa wanasubiri mshindi wa nusu fainali nyingine ya michuano hiyo itakayopigwa baadae leo kati ya mabingwa wa Ulaya na Dunia Hispania watakaochuana na Italia.

ABEL NA KISPANG WAJITOA TIMU YA WANARIADHA WA KENYA

BINGWA mara mbili wa dunia mashindano ya mbio ndefu Abel Kirui na mshindi wa medali ya shaba katika michuano ya olimpiki Wilson Kipsang wamejitoa katika timu ya wanariadha ya Kenya itakayoshiriki michuano ya riadha ya dunia itakayofanyika jijini Moscow. Makamu wa rais wa Chama cha Riadha cha nchi hiyo Paul Mutwii amedai kuwa Kurui aliwafahamisha kwamba amejitoa kwasababu ya kusumbuliwa na majeraha wakati Kipsang yeye amewaambia kuwa ana majukumu mengine. Kirui ambaye alishinda taji la dunia la mbio ndefu mwaka 2009 na 2011 amekuwa akisumbuliwa jeraha la kifundo cha mguu wake wa kulia na anatarajiwa kukaa nje ya uwanja kwa kipindi cha wiki sita. Kuziba nafasi hizo Mutwii amesema wamewaita Mike Kipyego ambaye alishinda mbio za marathon jijini Tokyo mwaka jana, Bernard Kipyego mshindi wa medali ya fedha mbio za nusu marathon 2009 na bingwa wa mbio za marathoni za Paris Peter Some. Kikosi cha mwisho kitakachokwenda Moscow kitatajwa mwezi ujao baada ya kufanyika mbioza mchujo.

JUVESTUS YATANGAZA RASMI KUMSAJILI TEVEZ

KLABU ya Juventus ya Italia jana ilimtangaza rasmi kumsajili mshambuliaji nyota wa kimataifa wa Argentina, Carlos Tevez kutoka timu ya Manchester City kwa mkataba wa miaka mitatu. Taarifa zinadai kuwa klabu yenye maskani yake katika jiji la Turin wamelipa kiasi cha paundi milioni 10 kwa nyota huyo mwenye umri wamiaka 29. Lakini Tevez atatakiwa kumaliza adhabu yake ya kutumikia jamii kwa saa 250 ili kuondoka jijini London salama na kuepuka kuburuzwa tena mahakamani. Tevez alikatisha likizo yake huko Amerika Kusini na kupanda ndege kuelekea Italia jana lakini pia atatakiwa kumaliza adhabu yake aliyopewa na mahakama ya Macclefield April mwaka huu kwa kuendesha huku akiwa amefungiwa kufanya hivyo.

Tuesday, June 25, 2013

VALCKE-ASEMA BRAZIL NDIO MAHALA PA KOMBE LA DUNIA"

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA, Jerome Valcke amesema kuwa hawana mpango wa kubadili mahali patakapochezwa michuano ya Kombe la Dunia mwakani. Valcke alibainisha kwamba michuano hiyo itafanyika nchini Brazil katika miji 12 kama ilivyopangwa na hakuna mpango mwingine wowote wa kuhamisha mashindano hayo kwenda sehemu nyingine. Kauli ya Valcke imekuja kufuatia maandamano ambayo yamekuwa yakiendelea nchini humo wakati huu wa michuano ya Kombe la Shirikisho wakipinga gharama kubwa za matayarisho ya Kombe la Dunia wakati wananchi wake wana hali duni katika maisha yao ya kawaida. Valcke pia alipinga kauli ya Waziri wa Michezo wa Brazil, Aldo Rebelo aliyekuwa amekaa pembeni yake katika mkutano na waandishi wa habari aliyedai kwamba kuna nchi zimeonyesha nia ya kuwa mwenyeji wa mashindano hayo kama Brazil ikijitoa. Katibu mkuu huyo amesema hajapokea ofa yoyote kutoka katika nchi yoyote duniani kutaka kuandaa michuano hiyo ya 2014 na kumuondoa hofu Rebelo ambaye alidai amesoma katika vyombo vya habari kwamba nchi za Marekani, Uingereza, Ujerumani na Japan zinamendea nafasi hiyo.