Wednesday, May 7, 2014

MAMBO YAIVA,RAIS MPYA SIMBA SC KUPATIKANA JUNI 29

Kamati ya uchaguzi ya Simba imepanga uchaguzi mkuu wa klabu hiyo kufanyika juni 29 mwaka huu baada ya msajili wa vyama vya michezo na klabu kuipitisha katiba yao iliyofanyiwa marekebisho.
DSC_0027 Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya Simba yalipopo mtaa wa Msimbazi Kariakoo, jijini Dar es salaam leo mchana, mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Simba sc, mwanasheria na wakala wa wachezaji wa FIFA, Dkt. Damas Ndumbaro amesema kamati yake imekutana jana na kuamua tarehe hiyo ya uchaguzi ili kupata rais mpya, makamu wa rais na wajumbe wapya wa kamati ya utendaji.
“Kamati yangu ina watu makini na wenye uadilifu mkubwa. Pia wana mawazo ya kuijenga klabu ya Simba”.
“Jana tulikutana na kupanga ratiba ya uchaguzi. Hatutakuwa na huruma na watu watakaoenda kinyume na kanuni za uchaguzi”. Alisema Ndumbaro.

Ndumbaro alisema kuanzia mei 9 mwaka huu mchakato wa kuanza kutoa fomu kwa watu wenye nia ya kuwania nafasi za uongozi utaanza rasmi, na siku ya kurudisha fomu ni mei 14 mwaka huu.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA TASWA

WIKI iliyopita kulifanyika Mkutano Mkuu wa Chama cha Kimataifa cha Waandishi wa Habari za Michezo (AIPS) jijini Baku, Azerbaijan.
Mkutano huo ulishirikisha viongozi wa vyama 116 vya waandishi wa habari za michezo duniani, ambapo Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), kiliwakilishwa na Katibu Mkuu, Amir Mhando.
 
amir-mhandoKatika mkutano huo msisitizo mkubwa umewekwa kwa nchi wanachama kutilia mkazo program za kuwaendeleza waandishi chipukizi wa habari za michezo, lakini pia AIPS yenyewe nayo pamoja na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Afrika (AIPS-Afrika) vimechukua jukumu la kusaidia kwa wale watakaokidhi vigezo wanavyohitaji.
 
Hivyo kila nchi mwanachama itatuma wasifu wa majina ya wanahabari chipukizi wasiozidi watano, ambao AIPS yenyewe itaangalia wale watakaofaa na kuwaandalia mafunzo baadaye mwaka huu.
 
Kwa upande wa AIPS Afrika yenyewe itaendesha mafunzo kwa wanahabari chipukizi 25, ambayo yatafanyika Morocco, lakini kipaumbele cha kwanza kitakuwa kwa nchi 16 zitakazocheza fainali za mataifa ya Afrika mwakani nchini humo na nafasi zingine zitabaki kwa nchi ambazo hazitaenda Morocco.
 
Mafunzo ni ya wazi kwa waandishi wowote chipukizi wasiozidi umri wa miaka 25, hata wale waliopo kwenye vyuo vya uandishi wa habari wataruhusiwa kuomba. Tanzania imewahi kupata nafasi moja mwaka 2011, ambapo Mwita Mwaikenda wakati huo akiwa mwanafunzo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alishiriki mafunzo hayo yaliyoandaliwa na AIPS akiwa miongoni mwa Waafrika watatu tu waliopata nafasi hiyo.
 
Utaratibu kuhusiana na suala hili utaelezwa vizuri baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya TASWA kitakachofanyika Jumatatu wiki ijayo kujadili masuala mbalimbali.
 
B: Ziara Uganda
Kulifanyika kikao cha viongozi wa nchi wanachama wa AIPS ambao wanatoka Afrika Mashariki, ambapo nchi za Burundi, Kenya, Tanzania na Uganda zilishiriki na kukubaliana kufanyike ziara ya kimafunzo itakayohusisha waaandishi wa habari za michezo Septemba 25-29 mwaka huu Kampala, Uganda. Rwanda licha ya kutoshiriki mkutano wa AIPS, lakini tulikubaliana nayo ialikwe.
Katika makubaliano hayo kila nchi itakuwa na washiriki wasiopungua 20 na wasiozidi 35, ambapo pia litafanyika kongamano kuhusiana na masuala mbalimbali ya waandishi wa habari za michezo kwa ukanda huo na siku ya mwisho litafanyika bonanza la michezo mbalimbali. Taarifa zaidi za ziara hiyo itatolewa siku za usoni.

C; Ushirikiano wa kimafunzo
 Baadhi ya nchi zilizoshiriki mkutano huo wa 77 wa AIPS, zilikubaliana kuanzisha utaratibu wa kubadilishana utaalamu wa kitaaluma kwa nchi mbalimbali, kwa kuwatoa baadhi ya wanahabari kwenda nchi zilizo katika makubaliano hayo kujifunza kwa gharama za nchi mwenyeji.
 
Hata hivyo makubaliano hayo, yataanza kufanya kazi baada ya kila nchi kupata baraka za Kamati ya Utendaji na kutuma majibu kwa waratibu kwamba wanaafiki. Kamati ya Utendaji ya TASWA katika kikao chake kijacho hilo litakuwa moja ya ajenda.

KINDA ANAEKIPIGA UJERUMANI AOMBA KUITWA STARS

Mwanandinga Kinda anayekipiga barani ulaya soka ya kulipwa Ujerumani, Charles Mishetto ameomba kuitwa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars aisaidie katika kampeni za kuing’oa Zimbabwe.
Hatua hiyo inakuja baada ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) kuikubalia TP Mazembe ya DRC ambayo imegoma kuwaachia Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu kuitumikia Taifa Stars katika mechi ya kuwania kushiriki fainali zijazo za Afrika (AFCON) dhidi ya Zimbabwe.
FIFA imesema klabu hazitashurutishwa kuwaachilia wachezaji wao ili washiriki mechi za kufuzu kwa michuano hiyo itakayofanyika Morocco mwakani, kwa sababu ipo nje kalenda ya mechi za shirikisho hilo.
Boniface Wambura, Ofisa Habari na Mwasiliano wa  TFF amesema kuwa wawili hao hawatakuwamo kwenye kikosi cha kovha
mpya Mholanzi Mart Nooij kitakachoivaa Zimbabwe mwishoni mwa wiki ijayo kwa vile wanahitajika kwenye klabu yao.
Mechi za kuwania kufuzu AFCON zitafanyika Mei 16-18, tarehe ambayo haipo kwenye ratiba ya FIFA na kwa hivyo haitakuwa lazima wachezaji wa klabu kuruhusiwa kuondoka.
Hata hivyo, michuano ya makundi itakayoshirikisha Ghana, Nigeria na Cameroon, zitakuwa katika tarehe iliyoidhinishwa na FIFA , ikimaanisha kuwa klabu vya soka kote duniani lazima ziwaruhusu wachezaji wao kushiriki mechi hizo.
Mbali na Samata na Ulimwengu, wachezaji kama Edward Sadomba, wataathiriwa na mgongano wa tarehe zilizo kati ya mechi za kufuzu zitakazofanyika 2015 na michuano ya klabu. Sadomba atahitajika kwa wakati mmoja na klabu yake ya Al Ahli Benghazi pamoja na timu yake ya taifa Zimbabwe itakayokipiga dhidi ya Taifa Stars.
Lakini FIFA lilikaririwa na BBC juzi likieleza kuwa wachezaji wanaweza tu kuondoka ikiwa maafisa wa klabu na mashirikisho ya nchi husika wanaweza kukubaliana.

Tuesday, May 6, 2014

TFF KUANZISHA MFUKO WA MAENDELEO TENGA M/KITI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeazimia kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu Tanzania (TFF Development Trust Fund).
Uamuzi wa kuanzisha mfuko huo umepitishwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya TFF iliyokutana Mei 3 mwaka huu jijini Dar es Salaam ambapo madhumuni yake ni kutafuta vyanzo vya rasilimali za kuendeleza programu za mpira wa miguu Tanzania.
Mfuko huo utakaokuwa chini ya uenyekiti wa Rais aliyepita wa TFF, Leodegar Tenga utatafuta rasilimali za kuendeshea michuano ya Taifa na kimataifa ya wavulana na wasichana kwa vijana wenye umri chini ya miaka 13, 15, 17 na 19.
MALINZI_N_HAYATOUPia kuendeleza maeneo ya ardhi kote Tanzania ambayo ni mali ya TFF kwa kujenga vituo vya michezo (sports centres), kutafuta rasilimali za kutoa mafunzo kwa makocha, marefa, madaktari wa tiba ya michezo na viongozi (administrators).
Majukumu mengine ya mfuko huo ni kuagiza na kusambaza vifaa vya michezo hasa kwa watoto wadogo (grassroots) na vijana.
Mfuko huo utazinduliwa Oktoba 8 mwaka huu ambayo ni siku ya kilele cha Tanzania kutimiza miaka 50 ya uanachama wake katika Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).
Mbali ya Tenga, wajumbe wengine wanaounda bodi ya mfuko huo ni Mwenyekiti wa zamani wa Simba, Ayoub Chamshama, Katibu Mkuu wa zamani wa TFF, Fredrick Mwakalebela, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha, Tarimba Abbas na Mbunge wa Viti Maalum, Zarina Madabida.
MWINYI KAZIMOTO ATUA TAIFA STARS
Kiungo mshambuliaji wa timu ya Al Markhiya ya Qatar, Mwinyi Kazimoto amewasili nchini kujiunga na kikosi cha Taifa Stars kinachojiandaa na mechi ya michuano ya Afrika dhidi ya Zimbabwe.
Kazimoto ambaye amewasili nchini jana (Mei 5 mwaka huu) anatarajia kusafiri leo (Mei 6 mwaka huu) kwenda Tukuyu mkoani Mbeya ambapo Taifa Stars imeweka kambi yake chini ya Kocha Mart Nooij kujiandaa kwa mechi hiyo.
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager juzi (Mei 4 mwaka huu) ilicheza mechi ya kirafiki na Malawi (Flames) ikiwa ni sehemu ya maandalizi kabla ya kuikabili Zimbabwe (Mighty Warriors). Mechi hiyo dhidi ya Flames ilichezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine na kumalizika kwa suluhu.
WACONGO KUCHEZESHA MECHI YA NGORONGORO HEROES
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC) kuchezesha mechi kati ya Tanzania (Ngorongoro Heroes) na Nigeria.
Mechi ya mchujo kusaka tiketi ya kucheza Fainali za 19 za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 zitakazofanyika mwakani nchini Senegal itachezwa wikiendi hii jijini Dar es Salaam.
Waamuzi hao wataongozwa na Jean-Jacques Ndala Ngambo atakayesaidiwa na Oliver Safari Kabene, Nabina Blaise Sebutu na Mupemba Ignace Nkongolo. Kamishna wa mechi hiyo namba 37 ni Poiret Antoine Ralph Danny kutoka Shelisheli.
BONIFACE WAMBURA
OFISA HABARI NA MAWASILIANO
SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)

Monday, May 5, 2014

UCHAHUZI WA SIMBA SASA MAMBO YAMEIVA BAADA YA KATIBA KUKAMILIKA.



UCHAGUZI mkuu wa klabu ya Simba sasa umeanza kuwadia baada ya Katiba ya timu hiyo kukamilika huku Kamati ya uchaguzi ikitarajiwa kukutana kesho kwa ajili ya kujadili tarehe rasmi ya kuanza mchakato wa uchaguzi huo.
Kamati ya uchaguzi ya klabu hiyo chini ya Mwenyekiti wake Damas Ndumbalo inatarajia kukutana kesho, kujadili mchakato mzima wa uchaguzi wa klabu hiyo ambao awali ulipangwa kufanyika mwishoni mwa wiki iliyopita.
Katiba ya Simba ambayo imefanyiwa marekebisho tayari imekabidhiwa jana kwa uongozi wa klabu hiyo kutoka kwa Serikali baada ya kupitiwa kifungu kwa kifungu na kuridhika nayo.
 Awali katiba hiyo ilionekana kuwa na mapungufu na kulazimisha kuipitia upya ili kuondoa mapungufu hayo, huku Mkurugenzi wa Michezo Leornad Thadeo akionekana kufanya kazi nzuri baada ya Simba kuirejesha Ijumaa ya wiki iliyopita.
Akizungumza na Waandishi wa Habari mjini Dar es Salaam leo, Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga, amesema kuwa tayari wamekabidhiwa Katiba ambapo kesho watakutana na kamati ya Uchaguzi kupanga mchakato mzima wa uchaguzi Mkuu wa Klabu hiyo.
Kamwaga amesema, baada ya kamati kukutana leo, taratibu nzima za mchakato huo, zitawekwa wazi kesho, na kuwapa fursa wagombea kuanza mchakato huo.
Alisema kuwa katiba yao imepitisha kuwepo kwa Kamati ya Maadili na Rufaa ambazo Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage atazitangaza wiki ijayo huku pia katiba ikipendekeza kuwepo kwa mgombea mmoja mwanamke wa kuchaguliwa.
Kamwaga alisema, vipengele vyote vimepita katika katiba yao, isipokuwa cha ibara ya 26(4) kuhusu sifa za mgombea.
“Katiba ya sasa ni lazima katika wagombea watano wa kamati ya utendaji nafasi moja awepo mwanamke, hivyo basi nawaomba wanawake mwenye sifa wajitokeze kwa wingi kuwania uongozi ndani ya Simba, na pia wanaweza hata wakawa watatu, lakini nafasi moja ni lazima

AZAM FC YAVUNJA MKATABA NA KONE WAMO AZIZI NA MWAIPOPO

UONGOZI wa klabu ya Azam FC umefikia makubaliano ya kuvunja Mkataba na mshambuliaji kutoka Ivory Coast, Ismail Kone ambaye alikuwa anamaliza Novemba mwaka huu.
Pande zote mbili zimefikia makubaliano na mchezaji huyo amepewa haki zake na kurejea nchini mwao. Aidha, Azam FC inawashukuru kwa mchango wao, wachezaji wake wanne, Jabir Aziz, Ibrahim Mwaipopo, Malika Ndeule na Omar Mtaki kwa kipindi chao chote walichoitumikia klabu hiyo.
Wanne hao wamemaliza mikataba yao na hawataongezewa- klabu inawashukuru kwa mchango wao kwa kipindi chote tangu wajiunge nayo. Azam FC pia imepokea na kuyakubali maombi ya wachezaji wake wawili, Samih Haji Nuhu na Luckson Kakolaki kustaafu kwa sababu mbalimbali.
Nuhu anasumbuliwa na maumivu ya goti ambalo hana matumaini ya kupona karibuni, wakati Kakolaki ameamua kustaafu ili achukue mafunzo ya ukocha. Klabu
imempa ajira ya kudumu Nuhu katika moja ya viwanda vyake, wakati Kakolaki ameingizwa kwenye benchi la Ufundi la akademi ya klabu.
Tayari klabu imekamilisha usajili wa wachezaji wapya watatu, ambao ni washambuliaji Didier Kavumbangu wa Burundi, Ismaila Diarra kutoka Mali na mzalendo Frank Domayo.
Usajili wa Kavumbangu na Diarra unafanya Azam iwe na wachezaji watano wa kigeni, wengine wakiwa ni Kipre Herman Tchetche na Kipre Michael Balou, ndugu wawili na pacha kutoka Ivory Coast na Mganda Brian Umony.
Azam chini ya kocha wake, Mcameroon Joseph Marius Omog imepanga kuboresha zaidi kikosi ili msimu ujao iweze kupata mafanikio zaidi katika Ligi ya Mabingwa Afrika na kutetea ubingwa wa Bara.

Sunday, May 4, 2014

STARS YATOA SARE NA MALAWI MECHI YA KIRAFIKI-SOKOINE

Kikosi cha Taifa Stars, chini ya Kocha mpya wa Mart Nooij leo amekiongoza kikosi chake kutoka sare ya bao 0-0 dhidi ya Malawi katika mechi ya kirafiki iliyochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, leo.


Nooij raia wa Uholanzi alikipanga kikosi chake leo kikiongozwa na wachezaji wengi wazoefu kilishambulia zaidi lakini hakikuweza kupata bao kutoka na kukosa mawasiliano mazuri katika safu ya ushambuliaji.
Hata hivyo Malawi nao walijibu mashambulizi katika kipindi cha pili  lakini hawakuweza kupata bao ambapo katika mtanange huo mashabiki wengi mashabiki mbalimbali mkoani mbeya wamejitokeza kuiunga mkono stars ya Mart Nooij.