Friday, May 24, 2013

WENYEVITI WA FA NDIYO WASIMAMIZI RCL WIKIENDI HII

WAKATI Mechi za kwanza za raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) zinachezwa wikiendi hii, Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imesisitiza kuwa wasimamizi wa mechi za ligi hiyo ni wenyeviti wa mikoa wa vyama vya mpira wa miguu.

Kamati hiyo chini ya uenyekiti wa Ramadhan Nassib ilikutana jana (Mei 23 mwaka huu) kupitia ripoti za makamishna kwa mechi za raundi ya kwanza ya RCL iliyomalizika wikiendi ya Mei 18 na 19 mwaka huu.

Kuhusu viwanja vinavyotumika kwa ligi hiyo, Kamati imesema vitaendelea kuwa vile vya makao makuu ya mikoa, na kwa vile vilivyokuwa vimeombwa vifanyiwe marekebisho ili viweze kukaguliwa kwa ajili ya RCL msimu ujao. Pia imeitaka mikoa kuendelea kuboresha viwanja vinavyotumika sasa, lakini vina upungufu.

Vilevile Kamati imebaini kuwa zimekuwepo pingamizi kuhusu usajili wa wachezaji ambapo imesema haiwezi kujadili pingamizi hizo kwa vile mikoa yote haikuwasilisha usajili wa wachezaji wa klabu husika uliofanyika mikoani kama ilivyoagizwa na kuelekezwa na TFF.

Hata hivyo, Kamati imeitaka mikoa ambayo klabu zao zimefanikiwa kuingia raundi ya pili kuwasilisha usajili huo haraka.

Pia Kamati imebaini kuwa zipo baadhi ya klabu ambazo zimekata rufani kuhusu usajili wa baadhi ya wachezaji, na kusisitiza kilichowasilishwa ni pingamizi kwa vile kwa mujibu wa kanuni masuala ya uwanjani hayakatiwi rufani. Hivyo, Kamati imeshauri klabu zilizokata rufani zilirejeshewe ada zilizolipa kwa ajili hiyo.

Makamishna na waamuzi wanaosimamia mechi za RCL wamekumbushwa kuwa ili mchezaji aruhusiwe kucheza mechi ni lazima awe na leseni yake (kadi ya usajili), vinginevyo asiruhusiwe kucheza mechi husika.
Mechi za RCL zinaendelea wikiendi hii ambapo zote zitachezwa Jumapili (Mei 26 mwaka huu) isipokuwa mechi kati ya Friends Rangers ya Dar es Salaam na African Sports ya Tanga itakayochezwa Jumamosi (Mei 25 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi.

Nayo mechi kati ya Abajalo ya Dar es Salaam na Kariakoo ya Lindi iliyokuwa ichezwe Jumamosi kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam sasa itachezwa Jumapili kwa vile siku hiyo uwanja huo utatumika kwa mazoezi ya Taifa Stars.

Mechi nyingine za RCL zitakazochezwa Mei 26 mwaka huu ni Machava FC ya Kilimanjaro dhidi ya Mpwapwa Stars ya Dodoma kwenye Uwanja wa Ushirika mjini Moshi, Stand United FC ya Shinyanga itakuwa mgeni wa Magic Pressure ya Singida kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida.

Polisi Jamii ya Bunda mkoani Mara na Biharamulo FC ya Kagera zitaumana kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma. Mjini Kigoma kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika ni kati ya wenyeji Saigon FC na Katavi Warriors ya Katavi.

Nayo Kimondo SC ya Mbeya itakuwa mgeni wa Njombe Mji ya Njombe katika mechi itakayochezwa Uwanja wa Sabasaba mjini Njombe. Mechi za marudiano zitachezwa kati ya Juni 1 na 2 mwaka huu.

Timu zitakazofuzu kucheza raundi ya tatu zitacheza mechi za kwanza kati ya Juni 8 na 9 mwaka huu wakati mechi za marudiano zitakuwa kati ya Juni 15 na 16 mwaka huu.

SEMINA YA USAJILI- TMS KUFANYIKA MEI 25
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeandaa semina ya usajili kwa njia ya mtandao (Transfer Matching System-TMS) kwa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom kwa ajili ya msimu wa 2013/2014.

Semina hiyo itafanyika Jumamosi (Mei 25 mwaka huu) kwenye ofisi za TFF saa 3 kamili asubuhi ikishirikisha watu wawili kutoka kila klabu ambao ni TMS Manager, na ofisa mwingine wa klabu.

Klabu za ligi hiyo zinazotakiwa kuhudhuria semina ya usajili ni Ashanti United, Azam, Coastal Union, JKT Ruvu, Kagera Sugar, Mbeya City, Mgambo Shooting, Mtibwa Sugar, Oljoro JKT, Rhino Rangers, Ruvu Shooting, Simba, Tanzania Prisons na Yanga.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Thursday, May 23, 2013

CITY YAKANUSHA KUWAWINDA FALCAO NA NEYMAR

NEYMAR_THE_BRAZILIAN
MKURUGENZI MKUU wa Manchester City chief Ferran Soriano amekanusha taarifa kuwa wanahaha kuwasaini Masupastaa Radamel Falcao na Neymar.
Hivi karibuni kumezagaa ripoti kuwa Man City ni miongoni mwa Klabu zinazokimbiza saini za Straika wa Atletico Madrid, Radamel Falcao, na yule wa Santos ya Brazil, Neymar.
Falcao anawindwa na msululu wa Klabu zikiwemo Chelsea, Monaco na Real Madrid baada ya kung’ara sana kwa kuifungia Atletico Mabao muhimu kwa Misimu kadhaa.
Nae Neymar, anaewindwa na Klabu kubwa Barani Ulaya, anatarajiwa kuihama Brazil baada ya Nchi hiyo kuwa Mwenyeji wa Kombe la Dunia Mwaka 2014.
Hata hivyo, Soriano amekanusha kwa kutamka: “Neymar na Falcao? Habari hizo ni uongo, hawajawahi kuwa kwenye ajenda yetu!”
Vile vile, Soriano aliponda habari kuwa wanataka kumuuza Straika wao mahiri Serio Aguero, mwenye Miaka 24, huku Real Madrid ikitajwa kuwa ndio atatua.
Soriano amesisitiza: “Hatujawahi kufikiria kumuuza Aguero. El Kun ana furaha kubaki kwetu Mwaka huu!”

MESSI AFURAHIA KUVAA JEZI NAMBA 10 AKIWA KATIKA TIMU HIYO.

MSHAMBULIAJI nyota maarufu dunia wa klabu ya Barcelona Lionel Messi amesema anajisikia raha na heshima kubwa kuvaa jezi namba 10 akiwa katika klabu hiyo na kufuata nyayo za Ronaldinho na nyota wengine waliokuwa wakivaa jezi hiyo. Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Argentina alirithi namba ya jezi ya Ronaldinho wakati nyota huyo wa Brazil alipoondoka Barcelona kwenda AC Milan katika kipindi cha majira ya kiangazi mwaka 2008 na kudai kuwa ilikuwa na maana kubwa kwake wakati anaanza kuivaa. Messi amesema wakati anapewa jezi hiyo namba 10 alijisikia furaha kwa ni jezi ambayo imekuwa ikivaliwa na wachezaji waliofanya mambo makubwa katika klabu hiyo. Nyota huyo pia alielezea nia yake ya kutaka kuiongoza timu ya taifa ya nchi yake kunyakuwa Kombe la Dunia huku akitaka mataji zaidi katika klabu yake ya Barcelona.

MOURINHO PAMOJA NA RONALDO WAFUNGIWA MECHI 2.

Kocha wa Real madrid Jose Mourinho pamoja na nyota wa klabu hiyo Cristiano Ronaldo wamefungiwa mechi mbili za michuano ya Kombe la Mfalme baada ya kutolewa nje katika fainali dhidi ya Atletico Madrid. Mourinho mwenye umri wa miaka 50 alitolewa nje baada ya kumshambulia mwamuzi kwa maamuzi aliyotoa adhabu ambayo hataweza kuitumikia baada ya kutangaza kuondoka klabuni hapo mwishoni mwa msimu huu. Ronaldo mwenye umri wa miaka 28 alipewa kadi nyekundu baada kukutwa na hatia ya kumpiga teke la uso kwa makusudi mchezaji wa Atletico, Gabi. Wote wawili Ronaldo na Mourinho watakuwepo katika michezo miwili ya mwisho ya ligi ya Madrid.

TIMU YA TAIFA YA CAMEROON YAPATA KOCHA MPYA.

Timu ya taifa ya Cameroon imefanikiwa kupata kocha mpya  Volker Finke kuwa kocha mkuu wa timu hiyo huku kibarua chake cha kwanza Mjerumani huyo ni kuhakikisha timu hiyo inafuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil. Finke anachukua nafasi ya kocha wa muda wa timu hiyo Jean-Paul Akono ambaye aliwekwa hapo kuziba nafasi ya Denis Lavagne Septemba mwaka jana baada ya Mfaransa huyo kushindwa kuisaidia timu hiyo kufuzu michuano ya Mataifa ya Afrika 2012 na 2013. Kocha huyo mwenye umri wa miaka 65 aliwahi kuifundisha klabu ya SC Freiburg kuanzia mwak 1991 mpaka 2007 na atakuwa anafundisha kikosi cha timu ya taifa kwa mara ya kwanza baada ya kutemwa na timu ya Urawa Red Diamonds ya Japan na timu ya Cologne ya nchini kwake. Katika mechi za kufuzu Kombe la Dunia, Cameroon wako kileleni mwa kundi I wakiwa na alama sita katika mechi tatu walizocheza wakifuatiwa na Libya wenye alama tano, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo-DRC alama nne na Togo alama moja. Kazi yake ya kwanza Finke itakuwa ni kukiongoza kikosi cha timu ya taifa ya nchi hiyo katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Ukraine utakaochezwa jijini Kiev Juni 2 mwaka huu kabla ya kuhamishia nguvu zao katika mechi za kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Togo Juni 9, DRC Juni 16 na Libya Septemba 6 mwaka huu

CLUB YA SANTOS YAKATAA OFA YA PILI YA BARCA

MAKAMU wa rais wa klabu ya Santos ya Brazil, Odilio Rodrigues amedai kwamba wamekataa ofa ya klabu ya Barcelona ya Hispania kutaka kumsajili mshambuliaji wao nyota Neymar kwa mara ya pili. Katika siku za hivi karibuni Barcelona ndiyo pekee wameonyesha nia ya kumhitaji mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Brazil na kuripoti kuwa walitaka kuwapa Santos euro milioni 20 ili waweze kumiliki haki za mchezaji huyo kwa asilimia 55. Wakati mahasimu wao nao Real madrid wakiongeza mbio ya kumfukuzia mshambuliaji huyo, Barcelona walitoa kiasi hicho ili waweze kumaliza suala hilo lakini Rodrigues amesisitiza kuwa hawana haraka ya kumuuza Neymar kwa kiasi kidogo kuliko wanachotaka. Rodrigues alithibitisha kuwa ni kweli walipata ofa ya Barcelona kwa mara ya pili lakini waliikataa kwasababu hawakufikia kiwango walichokuwa wakikihitaji. Neymar katika siku karibu ameweka wazi nia yake ya kubakia Santos mpaka baada ya michuano ya Kombe la Dunia 2014, ingawa uhamisho wa kwenda barani Ulaya katika kipindi hiki cha usajili unaonekana kama unaweza kuwepo.

FA CHADAI KUWA CARROL AJITOA TIMU YA TAIFA KUTOKANA NA MAJERUHI.

CHAMA cha Soka nchini Uingereza {FA} kimedai kuwa mshambuliaji wa kimataifa wa nchi hiyo, Andy Carroll amejitoa katika timu ya taifa kutokana na kuwa majeruhi. Carroll mwenye umri wa miaka 24 amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya kisigino baada ya kocha wa timu ya taifa Roy Hodgson kumuita katika kikosi chake ambacho kitacheza mechi mbili za kimataifa za kirafiki kati ya Ireland Mei 29 na Brazil Juni 2 katika Uwanja wa Maracana jijini Rio de Janeiro. Mshambuliaji huyo wa Liverpool amekuwa akicheza kwa mkopo katika klabu ya West Ham United msimu uliopita huku vyombo vya habari nchini Uingereza vikiripoti kuwa klabu hiyo imekubali kumchukua moja kwa moja kwa ada ya paundi milioni 15. Carroll anaungana na nahodha wa Liverpool Steven Gerrard na kiungo wa Arsenal Jack Wilshere kukosa mechi hizo za kujipima nguvu kabla ya mechi za kufuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014 dhidi ya Moldova na Ukraine Septemba mwaka huu.