CAF YATEU MUAMUZI KUTOKA MADAGASCAR KUCHEZESHA MECHI KATI YA TANZANIA VS UGANDA
Shirikisho la Mpira wa
Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Madagascar kuchezesha mechi
kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes) itakayochezwa
Jumamosi (Julai 27 mwaka huu) Uwanja wa Mandela ulioko Namboole nje
kidogo ya Jiji la Kampala. Waamuzi
wataongozwa na Kanoso Abdoul Ohabee wakati mwamuzi msaidizi namba moja
ni Andirvoavonjy Pierre Jean Eric. Mwamuzi msaidizi namba mbili ni
Jinoro Velomanana Ferdinand huku Andriamiharisoa Hubert Marie Bruno
akiwa mwamuzi wa mezani (fourth official). Kamishna
wa mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya mwisho kuwania tiketi ya
kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) ni Ismail Kamal
kutoka Ethiopia. Mechi
hiyo namba 38 itachezwa kuanzia saa 10 kamili jioni kwa saa za Afrika
Mashariki. Taifa Stars ilipoteza mechi ya kwanza iliyochezwa Julai 13
mwaka huu jijini Dar es Salaam kwa bao 1-0. Taifa
Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini jijini
Mwanza ikijiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo
mbili itacheza Fainali za CHAN mwakani nchini Afrika Kusini.